Utalii ndani ya majengo ya kihistoria Dar
- Ni majengo ambayo yalijengwa wakati ukoloni lakini yanatumika mpaka sasa.
- Yamebeba historia ya jiji hilo linalokua kwa kasi.
Dar es salaam. Safari ya kutalii katika jiji la kibiashara la Dar es Salaam bado inaendelea. Licha ya kutokupewa kipaumbele, jiji hili limesheheni vivutio vingi vya utalii ambavyo hupendeza macho sana.
Leo tunaangazia baadhi ya majengo yaliyobeba historia ya jiji hilo ambayo yanaendelea kutumika katika shughuli mbalimbali likiwemo la City Hall. Kuna nini kwenye majengo hayo? Endelea hapa chini:
City hall
Ni jengo kubwa la kale tangu 1903 lililobeba historia ya shughuli za utawala za mkoa wa Dar es salaam. Lilitumiwa na maafisa Wajerumani hadi waliposhindwa wakati wa vita ya kwanza ya dunia mwaka 1916. Baadae lilitwaliwa na Waingereza na kutumika kwa shughulu za kiutawala pia.
Kwa mujibu wa tovuti ya Makumbusho ya Taifa (NMT), Kwa sasa jengo hili linatumika kama ofisi ya Halmashauri ya jiji la Dar es salaam.
Linapatikana katika makutano ya barabara ya Sokoine na Morogoro, mita 800 kutoka kituo cha daladala cha Posta kupitia barabara ya Samora.
Msikiti wa Ibadhi
Ni jengo la kihistoria la kuabudia lilijengwa na wafanyabiashara wa Kiarabu waliofika katika misimu maalumu na wengine waliokaa moja kwa moja mwaka 1891.
Ukifika hapo utajifunza jinsi msikiti huo ulivyotumika katika harakati za kueneza dini ya Kiislamu wakati wa ukoloni nchini Tanzania hasa jijini Dar es Salaam. Msikiti huo unatumika kwa shughuli za ibada hasa na watu kutoka visiwani Zanzibar.
Unapatikana barabara ya Morogoro, mkabala na hospitali ya Ekenywa umbali wa kilomita 1.5 kutoka Posta.
Soma pia
Jengo la British Council
Ni jengo la kihistoria la shirika la Uingereza la mahusiano ya kitamaduni na fursa za elimu, lililojengwa mwaka 1930 na utawala wa Uingereza.
Jengo hilo lipo Mtaa wa Ohio karibu na Benki ya CRDB iliyopo jengo la Holland House mita 500 kutoka kituo cha daladala cha Posta mpya.
Kutembelea jengo hili utapata nafasi ya kujifunza historia ya namna ambavyo Waingereza wamesaidia maendeleo ya elimu, michezo, shule, na tasnia ya ubunifu.
Jengo la Maendeleo
Ni jengo la Shirika la Maendeleo la Taifa (NDC) lililoanzishwa mwaka 1962 kusimamia ukuaji na maendeleo ya viwanda nchini.
Utembeleapo mahali hapa utajifunza historia ya shughuli zilizoanzishwa na Serikali katika kuchochea maendeleo ya uchumi katika sekta zote katika vipindi tofauti.
Utapata pia taarifa muhimu zinazoelezea kuziba pengo la kufadhili miradi muhimu kwa kuchukua nafasi ya Shirika la Maendeleo la Kikoloni (CDC) lililoundwa mwaka 1950.
Ni rahisi kufika mahali hapa kutokea kituo cha daladala cha posta kwenda mtaa wa Ohio, umbali wa mita 700 kupitia barabara ya Maktaba Kuu.
Latest
