UNCTAD: Mfumuko wa bei watia dosari ukuaji wa uchumi duniani
- Mfumuko wa bei umerudisha nyuma mafanikio yaliyopatikana nusu ya kwanza ya mwaka huu.
- Thamani ya bidhaa na huduma zinatarajiwa kupungua kuelekea mwishoni mwa mwaka.
Dar es Salaam. Licha ya biashara duniani kukadiriwa kufikia thamani ya Dola za Marekani trilioni 32 mwaka 2022, mfumuko wa bei umerudisha nyuma mafanikio yaliyopatikana nusu ya kwanza ya mwaka huu, imeeleza ripoti mpya.
Ripoti hiyo ya ukuaji wa biashara duniani ya Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara duniani (UNCTAD) iliyotolewa Desemba 13, 2022 huko mjini Geneva, nchini Uswisi inaeleza kuwa ukuaji wa uchumi duniani uliporomoka na kufikia hasi katika nusu ya pili ya mwaka 2022.
UNCTAD inasema biashara ya bidhaa na huduma inatarajiwa kufikia Dola za Marekani trilioni 25 na dola trilioni 7 mtawalia, ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.
Kuporomoka kwa ukuaji wa uchumi kulianza robo ya tatu ya mwaka huu ambapo biashara ya bidhaa ilikuwa pungufu kwa asilimia moja ikilinganishwa na robo ya pili.
Katika ripoti yake hiyo kuhusu biashara, UNCTAD inasema ijapokuwa biashara ya huduma iliongezeka kwa asilimia 1.3 katika robo ya tatu ambayo ni mwezi Juni hadi Agosti, kwa ujumla thamani ya bidhaa na huduma zinatarajiwa kupungua kuelekea mwishoni mwa mwaka.
“Mvutano wa kijiografia, mfumuko wa bei na kuporomoka kwa mahitaji duniani vinatarajiwa kuwa na madhara kwa biashara duniani mwaka 2023,” imedokeza ripoti hiyo.
Miongoni mwa vigezo vinavyoleta changamoto ni makadirio ya ukuaji mdogo wa uchumi mwaka 2023 kutokana na bei ya juu ya nishati, viwango vya juu vya riba, mfumuko wa bei unaoendelea katika nchi nyingi na athari za vita nchini Ukraine.
Bei za bidhaa za vifaa na vyakula zinatarajiwa kupunguza mahitaji ya uagizaji wa bidhaa kutoka nje na hivyo kuchochea kupungua kwa kiwango cha biashara ya kimataifa.
Viwango vya juu vya deni la kimataifa na ongezeko la viwango vya riba vinaleta hofu kubwa ya uendelevu wa deni, na kuongeza shinikizo kwa serikali zenye madeni huku deni kwa mataifa kuedelea kukua.
Makubaliano ya hivi karibuni kama vile ubia wa kina wa kiuchumi kwenye ukanda wa Asia na Pasifiki, (RCEP) na eneo la biashara huru barani Afrika, (AfCFTA), UNCTAD imesema “yanapaswa kuwa suluhu na fursa ya kuongeza kasi kwenye mfumo wa kimataifa.”
Hata hivyo ukosefu wa uhakika na hatari zinatabiriwa kuendelea kuwa tishio kwenye mnyororo wa usambazaji wa huduma na bidhaa, lakini juhudi kuelekea uchumi usioharibu mazingira zinatarajiwa kuchochea ongezeko la mahitaji ya bidhaa endelevu kwa mazingira imesema UNCTAD huku ikipunguza mahitaji ya bidhaa zenye kiwango kikubwa cha hewa ya ukaa na nishati ya mafuta kisukuku.
Latest
