Ukosefu wa elimu, mirathi, sababu migogoro ya ardhi Mwanza.
- Sababu nyingine ni pamoja na migogoro ya mirathi na utunzaji mbaya wa kumbukumbu.
- Jumla ya malalmkiko 1,207 yawasilishwa kwa kipindi cha Januari na Februari 2024 pekee.
Mwanza. Serikali mkoani Mwanza imebainisha kuwa, ukosefu wa elimu sahihi ya ununuzi wa ardhi ni miongoni mwa mambo yanayochangia uwepo wa migogoro mingi ya ardhi jijini humo.
Kwa mujibu wa takwimu, Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa maeneo yanayoongoza kuwa na migogoro mingi ya ardhi ambapo katika kipindi cha Mwezi Julai hadi Februari 2024, malalamiko 1,207 ya ardhi yamesikilizwa.
Kwa mujibu wa Kamishna wa ardhi Mkoa wa Mwanza, Happyness Mtutwa kati ya migogoro hiyo, 86 pekee ndio ilitatuliwa na kuisha kabisa.
Mtutwa aliyekuwa akizungumza na Nukta Habari amesema migogoro hiyo inachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo wananchi kununua ardhi bila kujiridhisha uhalali wa eneo husika, migogoro ya familia pamoja na kutoweka kumbukumbu za ardhi vema.
“Ndio maana Waziri wa Ardhi anapenda kusisitiza kabla haujanunua eneo unapaswa kujihakikishia, ardhi sio kwamba unanunua shati kuwa popote unalipata, ni vema mnunuzi kuulizia kwa majirani ,uongozi wa Serikali za Mitaa na watu wengine,”amesema Mtutwa.
Mtuta ameongeza kuwa chanzo kingine cha migogoro ni wanafamilia kuwania eneo moja, jambo linalochangiwa kwa kiasi kikubwa na kutoandika wosia ambapo wao husubiri mpaka familia husika ikubaliane mmiliki ndipo mchakato wa kumilikishwa huanza.
Mikakati kumaliza migogoro ya ardhi Mwanza
Ili kukabiliana na migogoro hiyo, Mtutwa amesema kuwa Serikali itaendelea kupima maeneo mbalimbali, kufanya uthamini wa mali, kutoa hati, kukusanya mapato ya serikali, na kupanga maeneo kwa ajili ya uwekezaji.
“Katika suala hili la kutatua migogoro ya ardhi, tumekubaliana kufanyia kazi migogoro yote ambayo iliwasilishwa kwenye ziara za viongozi mbalimbali wa kitaifa, mkuu wa mkoa na wakuu wa wilaya pamoja kuendelea kusikiliza malalamiko mengine yatakayoendelea kuwasilishwa,” amesema Mtutwa.
Mkakati mwingine wa kuimarisha sekta hiyo ni usimamizi wa watumishi walioko chini namna watakavyosimamia masuala ya maadili, nidhamu za watumishi ili kuboresha huduma.