Ukopeshaji sekta binafsi waongezeka kwa asilimia 11.1 Tanzania
- Mikopo kwa sekta binafsi imeongezeka kwa asilimia 11.1 katika mwaka ulioishia Desemba 2019 ikilinganishwa na asilimia 4.9 katika kipindi kama hicho mwaka 2018.
- Ukuaji huo unatokana na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ikiwemo kuboresha mazingira ya biashara na sera zinazosimamia sekta ya fedha.
- Sehemu kubwa ya mikopo hiyo imeelekezwa katika shughuli za watu binafsi na biashara.
Dar es Salaam. Takwimu mpya za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zinaeleza kuwa mikopo kwa sekta binafsi imeongezeka kwa zaidi ya mara mbili ndani ya kipindi cha mwaka mmoja uliopita, huku sehemu kubwa ya mikopo hiyo ikielekezwa katika shughuli za watu binafsi na biashara.
Ripoti ya Mapitio ya Uchumi ya mwezi Januari 2019 (Economic Monthly Review) iliyotolewa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) hivi karibuni inaeleza kuwa mikopo kwa sekta binafsi imeongezeka kwa asilimia 11.1 katika mwaka ulioishia Desemba 2019 ikilinganishwa na asilimia 4.9 katika kipindi kama hicho mwaka 2018.
Hiyo ni sawa na ongezeko la zaidi ya mara mbili ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
BoT imeeleza katika ripoti hiyo kuwa ukuaji huo unatokana na hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ikiwemo kuboresha mazingira ya biashara na sera zinazosimamia sekta ya fedha.
“Kuongezeka kwa kasi ya ukuaji wa mikopo kwa sekta binafsi kulichangiwa na usimamizi thabiti wa sera ya fedha na jitihada zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali za kuboresha mazingira ya biashara,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo inayopatikana pia katika tovuti ya BoT.
Ripoti hiyo inaeleza kuwa sehemu kubwa ya mikopo kwa sekta binafsi imeendelea kuelekezwa kwa shughuli za watu binafsi au kaya ambazo zilipata wastani wa asilimia 29 ya mikopo yote ikifuatiwa na shughuli za biashara zilizokuwa na wastani wa asilimia 17.7.
Soma zaidi:
- Dk Mpango – Wastani wa pato la kila mtu waongezeka Tanzania
- Serikali kulenga shabaha tano za uchumi mwaka 2019-2020
- Ukopeshaji sekta binafsi waongezeka zaidi ya mara 10 Tanzania
Ukuaji wa mikopo katika shughuli zote kubwa za uchumi umeendelea kuongezeka, isipokuwa kwa shughuli za hoteli, migahawa na uzalishaji viwandani.
“Katika kipindi kilichoishia Desemba 2019, ukuaji wa mikopo ulishuhudiwa zaidi katika shughuli za kilimo, ujenzi, usafirishaji na mawasiliano,” inaeleza sehemu ya ripoti hiyo.
Sekta ya kilimo ndiyo ilishuhudia ukuaji mkubwa wa mikopo wa asilimia 90.1 ikifuatiwa na ujenzi (asilimia 72.6) na usafirishaji na mawasiliano (asilimia 14.6).
Mikopo inayoelekezwa katika sekta binafsi imekuwa chachu ya ukuaji wa shughuli za kiuchumi nchini kwa sababu hutumika kutunisha mtaji na ununuzi wa malighafi na utoaji huduma katika shughuli mbalimbali.
Hata wakati mikopo kwa sekta binafsi ikiongezeka, riba inayotozwa na benki za biashara imeongezeka pia, jambo ambalo linaweza kuwaumiza wakopaji na kuzifaidisha zaidi benki za biashara nchini.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, riba iliyotozwa kwenye mikopo iliyotolewa na benki mwezi Desemba 2019 ilikuwa asilimia 16.76 ikipanda kutoka asilimia 16.74 katika kipindi kama hicho mwaka 2018.
Benki kutoza riba kubwa, kunaweza kupunguza kasi ya wananchiwakiwemo wakulima kunufaika na huduma za kifedha zinazotolewa na taasisi hizo za fedha kwa ajili ya kujiletea maendeleo yao.