Uchafuzi wa mwaga: Tishio kwa uhai ndege wanaohama
Njia za ndege kuhama zinawapitisha katika miji mingi kote ulimwenguni ambayo ina mwanga bandia inayoweza kuathiri maisha yao. Picha| Unsplash/Karen Hammega.
- Mwanga huo unaotokana na shughuli za binadamu huwafanya wanyama kuchoka na kufa.
- Wadau waungana kutafuta suluhu ya kuwanusuru.
Dar es Salaam. Kila ifikapo Mei 14 kila mwaka ni Siku ya Kimataifa ya Ndege Wanaohama Duniani, kampeni ya kimataifa ambayo inalenga kuongeza ufahamu wa ndege wanaohama na haja ya ushirikiano wa kimataifa ili kuwahifadhi.
Kampeni hiyo yenye kauli mbiu isemayo “fifisha mwanga wa taa kwa ajili ya ndege usiku” huandaliwa kwa ushirikiano kati ya mikataba miwili ya Umoja wa Mataifa ya wanyamapori – Mkataba wa Uhifadhi wa Spishi zinazohama za Wanyama Pori (CMS) na Mkataba wa Uhifadhi wa Afrika (Eurasia) wa ndege wa maji wanaohama.
Umoja wa Mataifa (UN) kwa kushirikiana na wadau wengine wa wanyamapori wamesema mwanga bandia kwenye uso wa dunia Unaongezeka kila mwaka, jambo linalochangia kuhatarisha maisha ya ndege hao wanaohama kila mwaka.
“Kiasi cha mwanga bandia kwenye uso wa dunia kinaongezeka kwa angalau asilimia 2 kila mwaka na kinaweza kuwa kikubwa zaidi ya hapo baadaye,” imesema taarifa ya UN kuhusu ndege hao.
Amy Fraenkel, Katibu Mtendaji wa CMS amesema uchafuzi wa mwanga ni tishio kubwa na linaloongezeka kwa wanyamapori ikiwa ni pamoja na aina nyingi za ndege wanaohama.
“Kila mwaka, uchafuzi wa mwanga huchangia vifo vya mamilioni ya ndege. Unabadilisha mifumo ya asili ya mwanga na giza katika mfumo wa ikolojia. Unaweza kubadilisha mifumo ya uhamiaji ya ndege, tabia ya kutafuta chakula, na mawasiliano ya sauti,” amesema Fraenkel.
Amesema akiba ya nishati iliyopunguzwa inawaweka katika hatari ya kuchoka, kushambuliwa na kugongana na majengo ambapo wengi hufa.
UN imeeleza kuwa ongezeko la uchafuzi wa mwanga linachangiwa na uchafuzi wa anga ambapo zaidi ya asilimia 80 ya idadi ya watu duniani kwa sasa wanakadiriwa kuishi chini ya anga yenye mwanga.
Jacques Trouvilliez, Katibu Mtendaji wa Afrika-Eurasian (AEWA) wa mkataba wa ndege wa majini amesema ndege wengi wa aina mbalimbali, wanaofanya kazi usiku, wanapitia madhara ya uchafuzi wa mwanga.
Soma zaidi:
Jinsi ya kuwanusuru ndege hao
Kwa mujibu wa UN, miongozo kuhusu uchafuzi wa mwanga unaofunika kasa wa baharini, ndege wa baharini na ndege wanaohamahama iliidhinishwa na vyama vya CMS mwaka 2020.
Miongoni mwa mapendekezo yao, ni kwamba miongozo hiyo imeweka kanuni sita za utendaJI kazi bora wa mwanga na kutaka ifanyike tathmini ya athari za mwanga kwa mazingira na kwa miradi husika ambayo inaweza kusababisha uchafuzi wa mwanga.
Haya yanapaswa kuzingatia vyanzo vikuu vya uchafuzi wa mwanga kwenye maeneo fulani, aina za ndege wa porini ambao wanaweza kuathiriwa, na ukweli kuhusu ukaribu wa makazi muhimu na njia zinazotumika na nDege wahamao.
Miongozo mipya inayolenga ndege wa ardhini na popo wanaohama kwa sasa inaandaliwa chini ya CMS.
Itawasilishwa kwa wanachama wa CMS ili kupitishwa katika Mkutano wa 14 wa wanachama wa CMS mwaka 2023.