Tume ya uchunguzi matukio ya Oktoba 29 kuwasilisha ripoti Aprili 23
- Ni baada ya kuongezewa muda mara mbili.
- Watanzania 63,603 watoa maoni.
Arusha. Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya kabla na baada ya uchaguzi mkuu, inatarajiwa kukabidhi ripoti yake kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Alhamisi ya Aprili 23, 2026 baada ya kuongezewa muda mara mbili.
Ripoti hiyo huenda ikawa miongoni mwa mambo yanayosubiriwa kwa hamu kubwa na Watanzania, baada ya kuongezewa muda mara kadhaa tangu kuundwa kwa tume hiyo miezi mitano iliyopita.
Tume hiyo ilianza rasmi kutekeleza majukumu yake Novemba 20, 2025, mara baada ya kuzinduliwa na Rais Samia na ilitarajiwa kukamilisha kazi zake pamoja na kuwasilisha taarifa ndani ya kipindi cha siku 90, yaani kabla au ifikapo Februari 20, 2026.
Tofauti na matarajio ya wengi tume hiyo ilitangaza kuongezewa muda wa siku 42 na kutakiwa kuwasilisha ripori hiyo kabla au ifikapo Aprili 3, 2026 ahadi ambayo haikutekelezeka.
Aprili 7 mwaka huu tume hiyo ilitangaza kuongezewa tena muda wa siku 21 ikitakiwa kukamilisha kazi hiyo kabla au ifikapo Aprili 24, 2026 suala lilioibua maswali miongoni mwa wananchi na wadau wa masuala ya haki za binadamu nchini.
Kwa mujibu wa Jaji Chande Tume hiyo imepokea ushahidi kutoka kwa Watanzania 63,603 kwa njia mbalimbali.
Amesema ushahidi huo umepatikana kupitia mahojiano ya ana kwa ana yaliyohusisha watu 1,323, mashahidi wa viapo (affidavit) watu 553, madodoso yenye maswali bila kutaja majina ya wahusika watu 4,891, pamoja na mikutano ya makundi 202.
Latest