Teknolojia duni inavyokwamisha Watanzania kufaidika na mazao ya nyuki

March 26, 2022 10:52 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Ukosefu wa huduma za ugani na teknolojia duni huchangia.
  • Asilimia 20 ya rasilimali za misitu ndiyo hutumika kutengeneza asali na nta.

Dar es Salaam. Licha ya Tanzania kuwa na rasimali lukuki za misitu kwa ajili ya ufugaji wa nyuki, ni asilimia 20 ya rasilimali hizo ndiyo hutumika kutengeneza asali na nta, jambo linalowakosesha wafugaji wa wadudu hao mamilioni ya fedha.

Kwa mujibu wa mwongozo wa Taifa wa mafunzo ya ufugaji wa nyuki uliotolewa mwaka 2021 na Wizara ya Maliasili na Utalii unaeleza kuwa uzalishaji wa asali kwa sasa ni tani 30,393 kwa mwaka huku nta ikiwa ni tani 1,843. 

Mwongozo huo unaeleza kuwa, uzalishaji huo ni sawa na takriban asilimia 20 ya rasilimali zilizopo za misitu ambapo zikitumiwa vizuri kuna uwezekano wa kuzalisha asali takriban tani 138,000 na nta tani 9,200 kwa mwaka.

“Zaidi ya asilimia 50 ya mimea asilia nchini Tanzania huzalisha nekta au chavua au zote mbili ambazo ni lishe ya nyuki,” imeeleza sehemu ya mwongozo huo ambapo nyuki pia hukusanya nekta na chavua kutoka kwa mazao yanayolimwa kama vile alizeti, mikunde, miti ya machungwa, mkonge, kahawa, migomba na mahindi.

Uzalishaji huo duni wa mazao ya nyuki huchangiwa na ukosefu wa teknolojia ya kisasa ya ufugaji, jambo linalowakosesha fursa Watanzania kufaidika na soko la kimataifa.

“Tatizo siyo tu uzalishaji mdogo bali pia ubora na usalama wa bidhaa bado ni mdogo, idadi ya wafugaji nyuki bado ni ndogo, na ufugaji nyuki umesalia kuwa shughuli za wazee ingawa inatoa fursa kwa makundi yote ya watu na jinsia,” inaeleza sehemu ya mwongozo huo na kubainisha kuwa, 

“Huduma duni za ugani wa ufugaji nyuki pia zimechangia uelewa mdogo wa umma kuhusu viwanda vya bidhaa za nyuki ambavyo vingeweza kuajiri watu wengi na kuboresha maisha yao.”

Inakadiriwa kuwa nchini Tanzania, zaidi ya watu milioni 2 wameajiriwa kwenye mnyororo wa thamani wa ufugaji nyuki huku mchango wa sekta ya ufugaji nyuki katika pato la Taifa unaendelea kuwa chini ya asilimia moja ukilinganisha na uwezo uliopo.


Soma zaidi: 


Ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya nyuki, Wizara ya Maliasili na Utalii ilitoa mwongozo huo ambao umeanisha mbinu mbalimbali za ufugaji ambazo wakulima wakizutumia vizuri wanaweza kupata tija zaidi kwenye sekta hiyo.

“Uzoefu unaonyesha kuwa maeneo yanayotoa huduma za ugani ikiwemo maarifa na ujuzi  kwa ufanisi na uzalishaji wa sekta husika pia umeimarika,” umeeleza mwongozo huo na kubainisha kuwa huduma za ugani huharakisha uhamisho wa kiteknolojia na usimamizi mzuri wa shughuli za uzalishaji.

Umuhimu wa nyuki huenda zaidi ya matumizi ya kawaida kama chakula au pembejeo za viwandani. Nyuki huchangia kuboresha maisha ya watu kwa kuongeza chakula cha kaya, kipato na matengenezo ya mifumo ya ikolojia kupitia uchavushaji.

Mapema mwaka huu, Serikali ya Tanzania ilipokea Sh27 bilioni kupitia programu ya kuwezesha mnyororo wa thamani wa ufugaji nyuki iliyofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU).

Programu hiyo itanufaisha wananchi wa mikoa saba ya Tabora, Kigoma, Katavi, Singida, Shinyanga, Mkoa wa Kusini Pemba na Kaskazini Pemba.

Akizindua Programu hiyo  Februari 21 jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja alisema Serikali imefanya uchambuzi wa kitaalamu kubaini wilaya na vijiji vilivyomo ndani ya mikoa hiyo ambapo mradi huu utatekelezwa.

Programu hiyo itamarisha mifumo ya uzalishaji wa mazao ya nyuki, kuwezesha maeneo ya uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya nyuki katika maeneo husika.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...