TCU yasitisha udahili Shahada ya Udaktari, Chuo Kikuu Mwanza 2025/2026

December 2, 2025 3:05 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya chuo hicho kudahili na kusajili idadi ya wanafunzi mara kumi zaidi ya ile iliyoidhinishwa.

Dar es Salaam. Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imesitisha kibali cha udahili na usajili wa wanafunzi wa mwaka wa kwanza wa Shahada ya Udaktari wa Binadamu kwa Chuo Kikuu Mwanza (MzU) kwa mwaka wa masomo 2025/2026, baada ya kubainika ukiukwaji wa taratibu za udahili.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mtendaji wa TCU, Profesa Charles Kihampa, uamuzi wa TCU umefikiwa mara baada ya kufanya ukaguzi wa awali ambao ulibaini chuo hicho kimedahili na kusajili idadi ya wanafunzi mara kumi zaidi ya ile iliyoidhinishwa.

Aidha, TCU imeeleza kuwa kabla ya kufikia uamuzi huo ilitoa maelekezo kwa MzU kufanya marekebisho ya idadi ya wanafunzi waliodahiliwa, lakini chuo hicho kilishindwa kufanya marekebisho ambayo kwa mujibu wa tume ya idadi ya wanafunzi waliosajiliwa ni kubwa kuliko rasilimali zilizopo.

“Idadi husika ni kubwa kuliko uwezo wa chuo kimiundombinu ya kujifunzia na kufundishia ikiwamo idadi ya walimu waliopo,” imeeleza taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imefafanua kuwa mbali na kusitisha udahili, TCU pia imetoa kibali kwa wanafunzi wote wa mwaka wa kwanza waliodahiliwa na kuripoti chuoni hapo kuomba kuhamia katika vyuo vingine vilivyoruhusiwa kudahili wanafunzi wa programu ya Udaktari wa Binadamu au programu nyingine wanazozitaka, kwa mwaka huu wa masomo au miaka ijayo.

Aidha, MzU limeelekezwa kuwataarifu wanafunzi husika kuwa haitatoa masomo ya mwaka wa kwanza katika mwaka wa masomo 2025/2026 kutokana na kutokidhi taratibu za uendeshaji wa elimu ya chuo kikuu. 

“Chuo kinapaswa kuwasaidia wanafunzi hao kutafuta uhamisho kwenda vyuo vikuu vingine ambavyo viko tayari na vina uwezo wa kuwapokea,” imeeleza taarifa ya Profesa Kihampa.

TCU imetoa wito kwa wanafunzi walioathirika kuwa watulivu wakati mchakato wa uhamisho ukitekelezwa kwa ushirikiano baina ya chuo cha MzU na vyuo vitakavyowapokea wanafunzi, ambapo pia imeahidi kuhakikisha kuwa uhamisho utafanyika kwa haraka na ufanisi.

Mbali na hatua hizo, TCU pia imeunda kamati maalum ya wataalamu ili kuchunguza mchakato wa masuala ya kitaaluma katika Chuo Kikuu Mwanza na itaanza kazi mara tu baada ya zoezi la uhamisho kukamilika.

TCU imezisitiza kuwa itaendelea kutekeleza jukumu lake la kudhibiti ubora wa elimu ya juu nchini na kuchukua hatua stahiki ili kuhakikisha vyuo vyote vinazingatia sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa elimu ya chuo kikuu.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...