Tanzania yasaini mkataba na wawekezaji mradi wa gesi wa Sh70 trilioni
- Uamuzi wa mwisho wa kiuwekezaji katika mradi huo utakaojengwa mkoani Lindi unatarajiwa kufanywa mwaka 2025.
- Rais Samia ataka kuongezwa kwa kasi ya majadiliano katika kufikia hatua ya utekelezaji.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imeingia makubaliano ya awali na kampuni kubwa za uchimbaji mafuta duniani zikiwemo Equinor na Shell kwa ajili ya utekelezaji wa ujenzi wa mradi wa uchakataji na usimikaji gesi asilia wenye thamani ya Dola za Marekani 30 bilioni sawa na Sh70 trilioni.
Makubaliano hayo ya awali ya mkataba wan chi hodhi (HGA) yamefikia ikiwa ni zaidi ya miezi sita tangu Serikali irejee tena majadiliano na wawekezaji hao Novemba mwaka jana baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kueleza kuwa anataka kuona mradi huo ukiendelea kwa manufaa ya Watanzania na wawekezaji.
Katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dodoma Juni 11, 2022, kampuni hizo mbili zimeingia makubaliano hayo na Serikali kwa niaba ya wawekezaji wengine katika mradi huo ambao ni Ophir Energy, Exxon Mobil na Pavilion Energy.
Waziri wa Nishati January Makamba amesema hatua iliyofikiwa ni muhimu katika kutekeleza hatua nyingine za kutekeleza mradi huo wa kuchakata na kusindika gesi asilia utakaojengwa mkoani Lindi ikiwemo hatua ya umauzi wa mwisho wa kiuwekezaji (FID) mwaka 2025.
“Mazungumzo hayakuwa mapesi sana…kuna nyakati mambo yalitaka kuvunjika lakini ndiyo katika kuelekea kujenga…baadhi ya mambo yanayotakiwa yafanywe mbele yapo kwenye HGA hii,” amesema Makamba aliyeanza kuingoza wizara hiyo Septemba 2022.
Hatua ya kusaini mkataba huo uliosainiwa na wizara ya nishati pamoja na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC) pamoja na wawekezaji hiyo inatoa mwelekeo wa kutekeleza mradi huo ambao mazungumzo yake yalikuwa yamekwama kwa muda mrefu sasa.
- Maumivu: Bei ya mafuta zapaa
- Statoil yaja kivingine uchimbaji gesi Tanzania
- Mengi kuwekeza Sh68 bilioni uchimbaji wa mafuta, gesi Tanzania
Rais Samaia Suluhu Hassan amesema pamoja na kusaini mkataba huo wa makubaliano ya awali bado kuna safari ndefu kufikia uamuzi wa mwisho wa kiuwekezaji (FID) mwaka 2025 hivyo wote wanaohusika katika jambo hili waongeze kasi ya majadiliano.
Rais Samia amesema nchi zote zenye rasilimali za gesi zimepata mafanikio ya kiuchumi na ni mategemeo yake kuwa Tanzania nayo itapata maendeleo na ustawi wa watu wake kupitia rasilimali zake.
“Natumaini kwa kamuni za kimataifa zitatilia masuala haya katika majadiliano yanayoendelea ili kuhakikisha Tanzania inaingia vyema kwenye ramani ya dunai ya wazalishaji gesi na mazao ya gesi,” amesema kiongozi huyo wa juu wa nchi.
Wawekezaji hao wamesema wanaamini kuwa mradi huo utatekelezwa kutokana na hatua iliyopigwa hadi kufikia kusaini makubaliano ya awali hasa kipindi hiki ambacho mahitaji ya gesi asilia yamezidi kuongezeka duniani kutokana na ongezeko la watu na mahitaji ya nishati safi.
Makamu wa Rais wa kampuni ya Shell Tanzania, Jared Kuehl amesema gesi ya Tanzania itaweza kupata soko kwa sababu ina hewa ukaa kidogo na ipo karibu na soko kubwa la gesi la Asia.
“Gesi asilia kutoka Tanzania itaweza kufanikisha upatikanaji wa nishati safi isiyo na hewa ukaa nyingi…huu ni wakati muafaka kutekeleza mradi huu na kuhakikisha kuwa unafanikiwa kulifikia soko kutimiza mahitaji ya sasa ya gesi,” amesema Kuehl ambaye pia ni Mwenyekiti wa bodi ya kampuni hiyo.
dsfjhsgfjdhgjfghsghdfhgfgsgdhgfdsfgdshfgdshfgdh#
sfdsdfdsfdsfdsfdsdsfdsf