Tanzania kuongeza uwekezaji wa michezo shuleni
- Serikali yasema itaendelea kuibua vipaji vipya kupitia michezo.
- Kujenga miundombinu ikiwemo viwanja vya kisasa.
- Walimu watakiwa kuongeza kasi ya ufundishaji masomo ya michezo.
Dar es salaam. Katika kutambua mchango wa michezo katika kuibua vipaji vipya nchini Tanzania, Serikali imepanga kuendelea kuhamasisha ufundishaji wa michezo katika shule za msingi na sekondari.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa aliyekuwa akizindua mashindano ya Michezo na Taaluma kwa shule za Msingi Tanzania (Umitashumta) na Umoja wa Michezo kwa Shule za Sekondari Tanzania (Umiseta) leo Agosti 4, 2022 mkoani Tabora amesema Serikali itaendelea kuimarisha na kuboresha miundombinu ya michezo.
“Serikali imedhamiria kuboresha miundombinu ya michezo katika shule teule 56 nchini ikiwa ni wastani wa shule mbili kwa kila mkoa. Utekelezaji wa mradi huu kwa Mkoa wa Tabora tayari umeanza katika Shule za sekondari Tabora kwa wavulana na wasichana,” amesema Majaliwa.
Soma zaidi
- Jinsi ya kubaini kamera zilizofichwa kwenye nyumba ya kupanga, chumba cha hoteli
- Namna ya kupima ugonjwa wa rimoti kwa kamera ya simu
Majaliwa amesema pamoja na ujenzi wa viwanja, Serikali itajenga kumbi kubwa katika shule hizo zitakazotumika kwa kazi za sanaa na michezo ya ndani pamoja na kuajiri walimu wa michezo ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/22 walimu wa michezo 83 wameajiriwa.
Aidha, Majaliwa ametoa maagizo kwa viongozi wa elimu katika ngazi ya shule, kata, shehia, halmashauri na mkoa kufuatilia ufundishaji ili kuhakikisha wanafunzi wanapata umahiri uliokusudiwa katika masomo yote.
“Kila mwalimu ahakikishe anajiwekea malengo yake binafsi katika masomo anayofundisha na kuhakikisha kuwa hakuna mwanafunzi anayeshindwa kupata umahiri uliokusudiwa katika somo lake ifikapo mwishoni mwa kila mwaka,” amesema Majaliwa.
Mbali na kufungua mashindano ya michezo ya Umitashumta na Umiseta, kwa mwaka 2022, Waziri Mkuu amezindua vitabu vya miongozo na mikakati kwa ajili ya kuboresha elimu nchini unaolenga kuzipatia ufumbuzi changamoto zinazoathiri sekta ya elimu.
Latest