Tanzania kugeukia Tehama kubana matumizi
- Yasema matumizi hayo yatapunguza gharama za mikutano na Serikali
Dar es Salaam. Katika jitihada za kupunguza matumizi ya Serikali katika mikutano na safari, Waziri wa Fedha na Mipango, Mwigulu Nchemba amependekeza taasisi zote za umma kugeukia matumizi ya Tehama.
Ili kufanikisha matumizi hayo ya Tehama Waziri Nchemba amependekeza kumbi za mikoa na kumbi za wilaya ziwe na miundombinu ya mikutano ili kuwawezesha wabunge kushiriki mikutano na vikao vya mabaraza ya madiwani wakiwa mahali popote.
“Napendekeza matumizi ya mifumo ya Tehama iwe ni chaguo namba moja katika utekelezaji wa shughuli za serikali…mbona Bunge mmeweza,” amesema Waziri Nchemba wakati akiwalisha makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2022/23.
Kupitia miundombinu hiyo, amesema hata wabunge wataweza kushiriki vikao vya mabaraza ya Madiwani wakiwa Dodoma au hata nje ya nchi.
Sambamba na hilo waziri amepinga utaratibu wa viongozi waandamizi wa Serikali wakiwemo wakuu wa mikoa nchi nzima kukaa mahali na kusikiliza kikao kwa muda mfupi jambo linaloongeza mzigo kwa walipa kodi.
“Mtu anasafiri siku nne kuja kushiriki kikao cha nusu saa hadi masaaa matatu, anaacha kuhudumia wananchi na hatari zote za njiani na gharama zote kwa karne hii jambo hili siyo muafaka,” amesema.
Aidha Waziri Nchemba amesema suala la matumizi ya mtandao litasaidia watu wengi ikiwemo wafungwa kwa kuwa wengine wapo gerezani kwa sababu kesi zao zilishindwa kusikilizwa kwa wakati.
Latest
