Soko la fedha za kigeni tulivu Julai 14
- Dola ya Marekani imeendelea kuuzwa na kununuliwa kwa bei sawa na jana huku sarafu nyingine zikionyesha mabadadiliko madogo.
Dar es Salaam. Soko la fedha za kigeni limeendelea kuonyesha utulivu leo Julai, 14, 2026 huku baadhi ya sarafu zikionesha mabadiliko madogo katika benki za biashara nchini.
Takwimu za viwango vya kubadili fedha katika benki za CRDB na NMB zinaonyesha kuwa Dola ya Marekani imeendelea kuuzwa kwa Sh2,675 na kununuliwa kwa Sh2,595 kiwango sawa na kilichotumika jana Julai 13, 2026.
Hii inamaanisha kuwa Watanzania na wafanyabiashara wanaotumia Dola katika miamala yao wataendelea kutumia kiwango kile kile ambacho walitumia jana hali inayoleta utulivu wa kasi ya mfumuko wa bei katika soko hilo.
Kwa upande wa Pauni ya Uingereza imeonesha mabadiliko madogo ikishuka kiduchu katika benki zote mbili ambapo katika benki ya CRDB bei ya kununua imeshuka kwa Sh4.53 kutoka Sh3,374.17 iliyotumika jana hadi Sh3,369.64 leo huku bei ya kuuza ikishuka kutoka Sh3,674.17 hadi Sh3,669.17 sawa na punguzo la Sh6.
Katika benki ya NMB, Pauni ya Uingereza, imenunuliwa kwa Sh3,337 hii leo ikilinganishwa na Sh3,343 ya jana, ikiwa ni sawa na kushuka kwa Sh6, na wakati huo bei ya kuuza pia imeshuka kutoka Sh3,688 hadi Sh3,682, ikiwa ni sawa na punguzo la Shilingi 6.
Kwa upande wa sarafu za kikanda Shilingi ya Kenya na Uganda zimeendelea kuonyesha utulivu zikionyesha mabadiliko madogo dhidi ya Shilingi ya Tanzania.
