Siri matumizi ya jina, umiliki wa mali katika biashara ya ushirika
Katika mazingira ya sasa baadhi ya watu huanzisha biashara kwa mfumo wa ushirika. Hata hivyo, si wote hufahamu mambo mengi kuhusu aina hiyo ya biashara ambayo kwa kimombo huitwa “partnership”.
Katika sehemu ya kwanza ya makala hii tuliangazia baadhi ya mambo ya awali ya kuzingatia unapoingia katika ushirika kufanya biashara. Endelea…
Siri ya umiliki wa mali za ushirika
Ushirika au sio mtu hai mbele ya uso wa sheria kama ilivyo kwa kampuni. Sheria inatamka bayana kuwa ni watu hai pekee mbele ya sheria ndo wanawzeza kumiliki mali.
Partnership haina hadhi ya binadamu mbele ya macho ya sheria hivyo basi haiwezi kumiliki mali zake zenyewe. Kwa mujibu wa kifungu cha 195 cha sheria za mikataba (Law of Contract Act) mali za biashara ya aina hiyo ya huwa zinamilikiwa na wadau wa ushirika husika.
Ni lini matumizi ya jina la biashara ya ushirika yanakoma?
Hakuna mdau wa ushirika huu anaruhusiwa kutumia jina la partnership kwa shughuli zake binafsi. Matumizi yoyote ya jina la partnership yanatakiwa kufanywa kwa kupewa ruhusa maalumu au kwa makubaliano ya wadau wote.
Soma zaidi:
- Kabla ya kuingia katika biashara ya ushirika, zingatia haya
- Mo Dewji: Nilianzisha programu ya wajasiriamali haikufanikiwa
Je, mshirika katika biashara anaweza kufukuzwa?
Hakuna mshirika yeyote katika biashara husika anaruhusiwa kufukuza mshirika mwingine kwenye ushirika huo isipokua tu pale ambapo mkataba wa ushirika umeelezea kwa undani suala hilo. Mkataba huo ndiyo roho ya ushirika wenu.
Hii inamaanisha kuwa hakuna mwanachama mwenye nguvu zaidi ya mwenzake ndani ya ushirika huu kwa mujibu wa kifungu cha 199 cha sheria za mikataba.
Kifo cha biashara ya ushirika
Ushirika wa kibiashara ulizaliwa na kupewa cheti chake cha kuzaliwa lakini maisha yake yanaweza kufika mwisho na kuwa ndio kifo chake rasmi kwa njia mbalimbali kwa mujibu wa sheria. Njia hizo zinaweza kuwa kama zifuatazo kwa mujibu wa kifungu cha 212 cha sheria za mikataba.
- Wameamua kuhitimisha maisha ya ushirika wao
Hii inatokea pale ambapo malengo yaliyokusudiwa kwa ajili ya ushirika huo yamekua yameshafikiwa au pale ambapo muda uliowekwa kwa ajili ya ushirika huo unakua umekoma. Hivyo basi tangazo au taarifa ya kuvunjwa kwa ushirika huo itatolewa rasmi kwa wana ushirika na kuweza kuhitimisha ushirika huo.
- Mahakama
Ina uwezo wa kuhitimisha maisha ya ushirika kwa maombi ya mdau au baada ya ushirika huo kushindwa kukidhi vigezo vya kisheria. Kwa mfano, kufanya biashara haramu au kujihusisha na utakatishaji fedha. Wakati mwingine pale ambapo partner mmoja anapokua na ugonjwa wa akili mahakama inaweza kuingilia kati na kuvunja ushirika huu.
Endapo mahakama itakua na maoni kuwa ushirika huu unaendeshwa kinyume na sheria basi itaufuta na kuhitimisha safari ya ushirika huo.
Kabla ya kuingia kwenye biashara ya ushirika hakikisha umeelewa vema mambo yote yanayohusu uendeshaji wa aina hiyo ya biashara. Picha|Christina @ wocintechchat.com/Unsplash.
Kufa au kufilisika kwa mshirika
Ikiwa wana ushirika walikubaliana kuwa kifo au kufilisika kwa partner ndo itakua mwisho wa ushirika wao basi itakua hivyo.
Notisi ya kujitoa
Ikiwa mshirika mmoja anataka kujitoa kwenye ushirika husika anapaswa kuwajulisha wenzie kwa kuwapa notisi kwa mujibu wa kifungu cha 217 cha sheria za mikataba.
Angalizo
Kabla haujaingia kwenye ushirika hakikisha unasoma vizuri mkataba wa ushirika ili kuweza kujua haki za msingi za mwanachama kabla hujaingia mkenge. Kama tunavyohamu unaingia kwenye ushirika ili kuhakikisha maslahi yako na washirika wenzio yanatimizwa.
Mwandishi wa makala hii Hamza Yusufu Lule ni Wakili wa Mahakama Kuu na mahakama za chini Tanzania. Kwa mawasiliano zaidi kuhusu ushauri wa kisheria wasiliana naye kupitia Twiter: @Hamzaalbhanj Simu; 0717521700.