Si kweli: Wezi waiba basi la polisi mkoani Mbeya
- Jeshi la Polisi Latangaza kuwasaka waliosambaza taarifa hiyo.
Arusha. Ikiwa wewe ni mtumiaji wa mitandao ya kijamii huenda umekutana na taarifa ya wezi kuiba gari la polisi mkoani Mbeya, taarifa hizo sio za kweli.
Taarifa ya Wilbert Siwa, Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoani Mbeya iliyotolewa leo Machi 17, 2025 imekanusha kutokea kwa tukio hilo na kuwataka wannchi kuipuuzia
“Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linakanusha taarifa inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii inayosema “WEZI WAIBA BASI LA POLISI MKOANI MBEYA” na kuiomba jamii kupuuza taarifa hiyo kwani hakuna tukio kama hilo mkoani Mbeya.” imesema taarifa ya Siwa.
Habari hiyo iliyokuwa ikisambaa katika mitandao ya kijamii imechota hisia za watumiaji wengi wa mitandao hiyo kutokana na kutumia muundo na rangi zinatumika na chombo cha habari cha Milard Ayo.
Pamoja na hayo, imetumia picha ya gari ya polisi pamoja na nembo ya polisi katika muundo ambao chombo cha milard Ayo hutumia hivyo kuvutia watumiaji wengi wa mitandao hiyo.
Hata hivyo, Jeshi hilo limebainisha kuwa halina basi lenye namba PT 4037 kama zinavyosomeka kwenye picha mnato iliyoambatishwa kwenye taarifa hiyo huku likitangaza kuwasaka walioa taarifa hiyo.
“Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linaendelea na uchunguzi wa kuwabaini waliohusika na utoaji wa taarifa hiyo ya uzushi na kuleta taharuki kwa jamii ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi yao,” imesema taarifa ya jeshi hilo.
Latest



