Si kweli : Biopsia husababisha saratani kusambaa kwa haraka
- Wizara ya Afya yasema biospia ni njia salama, inayotambulika duniani kote katika kuthibitisha aina ya saratani.
- Yawataka wafanyabiashara wanaodai kutibu kwa njia ya asili kuacha kupotosha jamii, wananchi wanaaswa kutotegemea taarifa zisizothibitishwa.
Dar es Salaam. Kumekuwa na video inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii hususan Tiktok ikidai kuwa uchunguzi wa saratani ya matiti kwa kutumia biopsia husababisha saratani kuenea kwa kasi, taarifa ambayo si ya kweli.
Kupitia video aliyochapisha kwenye mtandao wa tiktok yenye jina dr_masipeti, dada huyo ambaye anajinasibu kuwa ni mtaalam wa tiba asili amewasihi watu wenye dalili ya saratani ya titi kutokubali kufanya uchunguzi kwa kutumia njia ya kitaalam ya biopsia kwa kudai kuwa inasababisha saratani kusambaa kwa haraka.
“Usirudie tena kufanya kitu kinaitwa biopsi, saratani ukienda kufanya biopsi inasambaa kwa spidi ya hali ya juu” amepotosha dada huyo kupitia akaunti yake ya TikTok.
Ukweli ni huu
Biopsia ni utaratibu wa kitabibu ambapo daktari huchukua kipande kidogo cha tishu au seli kutoka sehemu ya mwili ili kuchunguzwa maabara kwa lengo la kubaini uwepo wa saratani, aina ya uvimbe au magonjwa mengine.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) biopsia hufanyika kwa taratibu tofauti kulingana na eneo la tatizo, ambapo daktari anaweza kutumia sindano nyembamba kuvuta seli (needle biopsy), kuchukua kipande kidogo cha tishu kwa upasuaji mdogo au kutumia kifaa maalum kupitia mdomoni au sehemu nyingine ya mwili (endoscopic biopsy).
Kipimo hicho mara nyingi hufanywa kwa kutumia ganzi eneo husika ili kupunguza maumivu na husaidia kuthibitisha uwepo wa saratani, kubaini aina na hatua ya ugonjwa, kutambua maambukizi au mabadiliko yasiyo ya kawaida ya seli, ili kuwaongoza madaktari kupanga matibabu sahihi na kwa wakati.
Taarifa ya Wizara ya Afya iliyotolewa Machi 4, 2026 imefafanua kuwa taarifa ya mwanadada huyo kuhusu biospia ni upotoshaji unaoweza kuhatarisha maisha ya wagonjwa.
Aidha, wizara imefafanua kuwa mtu anayeonekana kwenye video inayosambazwa si mtaalamu wa tiba asili na wala hatambuliwi na baraza lolote la kitaaluma nchini.
“Baada ya ufuatiliaji tumegundua muhusika anajihusisha na biashara za bidhaa za kimtandao “network marketing” na wala hatakiwi kuelimisha jamii masuala ya afya,” imesema taarifa hiyo.
Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala limewaelekeza wanataaluma wa tiba hiyo, wafanyabiashara na wajasiriamali wote wa bidhaa mbalimbali wanaotoa elimu au kutumia bidhaa hizo waondoe matangazo yote yanayopotosha jamii, kwani yanaweza kuchelewesha wagonjwa kupata matibabu kwa wakati.
Wizara imewahimiza wananchi kutotegemea taarifa zisizothibitishwa, na badala yake kufika katika vituo rasmi vya afya vinavyotambulika kwa ajili ya uchunguzi na matibabu sahihi yanayotolewa na wataalamu waliothibitishwa.
Latest