Shilingi yaimarika dhidi ya Euro na Pauni yabaki tulivu dhidi ya Dola
- Ni fursa kwa wafanyabiashara wanaofanya miamala kwa kutumia sarafu hizo.
Dar es Salaam. Shilingi ya Tanzania imeanza wiki ikiwa imeimarika dhidi ya baadhi ya sarafu kuu za dunia, hususan Euro na Pauni ya Uingereza, huku Dola ya Marekani ikiendelea kubaki katika viwango vilevile ilivyokuwa mwishoni mwa wiki iliyopita.
Takwimu za viwango vya kubadili fedha katika benki ya CRDB na NMB zinaonyesha kiwango cha Dola ya Marekani hakijabadilika katika benki zote mbili. CRDB imeendelea kununua dola kwa Sh2,595 na kuuza kwa Sh2,675, wakati NMB nayo imebaki Sh2,595 kwa bei ya kununua na Sh2,675 bei ya kuuza.
Hata hivyo, Euro imeonyesha kushuka dhidi ya Shilingi. Katika Benki ya CRDB, kiwango cha kununua Euro kimeshuka kutoka Sh2,864.44 hadi Sh2,858, huku kiwango cha kuuza kikishuka kutoka Sh3,164.44 hadi Sh3,158. NMB pia imepunguza kiwango cha kununua Euro kutoka Sh2,880 hadi Sh2,872 na kiwango cha kuuza kutoka Sh3,152 hadi Sh3,142.

Pauni ya Uingereza (GBP) nayo imeendelea kupungua. CRDB imenunua Pauni kwa Sh3,386 kutoka Sh3,403.36 za Ijumaa, huku bei ya kuuza ikishuka hadi Sh3,686 kutoka Sh3,703.36. NMB nayo imepunguza kiwango cha kununua kutoka Sh3,367 hadi Sh3,349, ingawa kiwango cha kuuza kimepungua kwa kiasi kidogo kutoka Sh3,713 hadi Sh3,694.
Kwa sarafu za ukanda wa Afrika Mashariki, Shilingi ya Kenya imeendelea kubaki katika viwango vilevile katika benki zote mbili. CRDB imeendelea kununua kwa Sh16.87 na kuuza kwa Sh23.87, wakati NMB imeendelea kununua kwa Sh17.8 na kuuza kwa Sh22.4.
Shilingi ya Uganda imeonyesha mabadiliko madogo katika CRDB, ambapo kiwango cha kununua kimeshuka kutoka Sh0.69 hadi Sh0.685 na kuuza kutoka Sh0.74 hadi Sh0.735. NMB haijabadilisha viwango vyake, ikiendelea kununua kwa Sh0.63 na kuuza kwa Sh0.91.