Sh307 milioni zawaweka matatani watendaji 34 Kagera
- Maafisa wanne wamesimamishwa kazi huku Watendaji 30 wakikabidhiwa mikononi mwaka polisi na TAKUKURU.
- Wameshindwa kurejesha Sh307 milioni za mapato ya Halmashauri ya Biharamulo.
Dar es Salaam. Watumishi 30 katika Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo wakiwemo watendaji wa vijiji na kata leo wamekabidhiwa mikononi mwa polisi kwa kushindwa kurejesha Sh307 milioni zilizokusanywa kutoka vyanzo vya mapato ya ndani bila kupelekwa benki.
Mkuu wa mkoa huo Brigedia Jenerali Marco Gaguti amemwagiza Kamanda wa Polisi mkoani humo pamoja na Kamanda wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwakamata watendaji hao mara moja ili wakajibu tuhuma zinazowakabili.
“Nilikuja hapa nikatoa maelekezo kwa wale wote waliokuwa wanakusanya fedha kwa kutumia mashine za “Poss” bila kuzipeleka benki kuwa warejeshe fedha na nikawapa siku saba lakini fedha iliyorejeshwa ni asilimia 2.
“Hapa nina orodha ya watendaji 30 ambayo nampatia kamanda wa polisi kuhakikisha watu hao wanakamatwa popote walipo na wengine wanne hawa naagiza wasimamishwe kazi lakini wawe chini ya uangalizi wa kamati ya ulinzi na usalama ili kutoa ushirikiano,” amesema Brigedia Jenerali Gaguti leo Juni 23, 2020 wilayani humo.
Watumishi wa halmashauri hiyo waliosimamishwa kazi ni pamoja na aliyekuwa Kaimu mweka hazina Sospiter Makene, Maafisa Tehama Jastine Banula na Rogers Semukoko na Afisa Biashara Beatrice Gurusya
Zinazohusiana
Amesema watumishi wa umma wanatakiwa kuwa waadilifu na kuiogopa fedha ya Serikali na kuahidi kuwachukulia hatua wote watakaobainika wakifanya vitendo vya ubadhilifu na kutoa onyo kali kwa watendaji wa vijiji na kata mkoani humo kuhakikisha wanasimamia ukusanyaji wa mapato ya serikali bila kuleta “ujanja ujanja”.
Ikumbukwe kuwa, Gaguti amechukua uamuzi huo baada ya kutoa siku saba kwa watumishi hao kurejesha fedha hizo kwenye kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo kilichofanyika Juni 5, 2020 mwaka huu kilichokuwa kina lengo la kujibu hoja za Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali.
Latest
