Serikali yatoa matibabu bure kwa binti aliyechomwa moto Mwanza
- Yasema matibabu pamoja na dawa vitatolewa bure hadi pale atakapopona.
- Hali yake inazidi kutengemaa.
- Mkuu wa wilaya ya Misungwi, Johari Samizi ametoa wito kwa waajiri kuacha kujichukulia sheria mkononi.
Mwanza. Serikali ya Tanzania kupitia uongozi wa Hospitali ya wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza imetoa matibabu bure kwa Grace Joseph (17) aliyechomwa moto na mwajiri wake Christina Shiriri mwanzoni mwa wiki hii akituhumiwa kuiba Sh161, 000.
Mganga Mkuu wa Halmashauri ya wilaya ya Misungwi, Dk Clement Mwarabu aliyekuwa akizungumza na wanahabari amesema mgonjwa huyo ameungua kwa asilimia 20 hususani katika maeo ya tumbo, mikono na miguu na kutokana na hali hiyo hawezi kuchangia matibabu.
“Kwa hali aliyonayo(mgonnjwa) hawezi kuchangia kwa hiyo tumetoa msamaha gharama zote ni bure, Serikali inagharamia kupitia hospitali na Halmashauri ya Misungwi inatoa dawa zote labda zile zinazokosekana ndiyo ndugu wanaweza kununua nje,”amesema Dk Clement.
Soma zaidi:Ndugu wa aliyechomwa moto na mwajiri wake Mwanza, washinikiza hatua zaidi za kisheria
Ameongeza kuwa kwa sasa mgonjwa huyo anaendelea vizuri kulinganisha na hali aliyokuwa nayo awali wakati anafikishwa hospitalini hapo.
Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Misungwi, Johari Samizi ametoa wito kwa waajiri kuacha kujichukulia sheria mkononi kwani wanaweza kusababisha madhara makubwa zaidi.
Tukio la mfanyakazi huyo kuchomwa moto na mwajiri wake lilipotiwa Juni 5 mwaka huu na Kamanda wa polisi Mkoa wa Mwanza, DCP Wilbroad Mutafungwa na kueleza kuwa mtuhumiwa aliamua kufanya kitendo hicho akimtuhumu kuiba kiasi hicho cha fedha.
Hata hivyo Kamanda Mutafungwa amesema uchunguzi wa tukio hilo bado unaendelea, mtuhumiwa amekamatwa na atafikishwa mahakamani mara tu uchunguzi huo utakapokamilika.