Serikali, sekta binafsi zitakavyoshirikiana kufikia dira 2050
- Serikali yaahidi kuboresha mazingira ya biashara.
- Wafanyabiashara watakiwa kuongeza uzalishaji na ushindani.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania na sekta binafsi wameweka mkakati wa pamoja wa kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kupitia uwekezaji, uzalishaji, maendeleo ya viwanda, ajira na ujenzi wa uchumi shindani unaowanufaisha wananchi wote.
Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dk Tausi Kida aliyekuwa akizungumza leo Agosti 3, 2026, kwenye hafla ya uzinduzi wa nyezo za utekelezaji wa Dira ya 2050 amesema lengo la hatua hiyo ni kujenga ushirikiano wa kimkakati kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ili kuhakikisha dira hiyo inatekelezwa kwa ufanisi.
“Hii ni ishara ya wazi ya dhamira ya Serikali ya kuhakikisha kuwa Dira 2050 haibaki kuwa maono au waraka wa sera pekee bali inaanza kutekelezwa mara moja kupitia mfumo kamili ulioratibiwa na unaoweka misingi ya uwajibikaji, ufuatiliaji na ufuatiliaji wa matokeo,” amesema Kida.
Miongoni mwa nyenzo zilizozinduliwa ni Mpango Elekezi wa Maendeleo wa Muda Mrefu wa miaka 25, Mpango wa Nne wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP IV), Mwongozo wa Kitaifa wa Upimaji wa Matokeo ya Utekelezaji wa Mipango ya Maendeleo pamoja na Mkakati wa Mawasiliano wa Dira 2050.

Kupitia ushirikiano huo, Serikali imeahidi kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji, kuimarisha miundombinu ya kimkakati, kukuza viwanda, kuongeza thamani ya rasilimali na kuimarisha majadiliano na sekta binafsi ili kutatua changamoto zinazokwamisha ukuaji wa uchumi.
Kwa upande wa sekta binafsi imeahidi kuongeza uwekezaji, kuzalisha ajira zenye staha, kukuza ubunifu, kuimarisha biashara za wazawa na kuongeza mauzo ya bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na kimataifa.
Sekta binafsi ni nguzo muhimu katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku ikitarajiwa kuchangia takribani asilimia 70 ya utekelezaji wa malengo ya dira hiyo.
Mchakato wa kuandaa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ulianza rasmi mwaka 2023 baada ya Serikali kuanza maandalizi ya dira mpya itakayotoa mwelekeo wa maendeleo ya Tanzania kwa kipindi cha miaka 25 ijayo, baada ya kumalizika kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025.
Akizungumza katika hafla hiyo Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema ushirikiano huo ni muhimu ili kutumia nafasi ya Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji na usafirishaji barani Afrika.

Amesema Serikali itaendelea kuboresha miundombinu ikiwemo reli na mifumo ya usafirishaji, huku sekta binafsi ikitakiwa kuongeza nguvu katika uzalishaji na kutumia fursa zilizopo.
“Nataka kuahidi kwamba tutashirikiana kuijenga sekta binafsi. Nataka nione wawekezaji wetu wa ndani, wafanyabiashara wa ndani wanatoka nje ya mipaka yetu. Tunataka kufanya wengi zaidi kuwatafutia fursa na kuwawezesha muweze kutoka nje ya mipaka yetu,” amesema Rais Samia.
Akizungumzia dhamira yake ya kuendelea kutumikia taifa, Rais Samia amesema yeye ni mshumaa tu, kazi yake ni kuwaka kutoa mwanga huku akitetetea lengo umati ufurahi.