Serikali kujenga uwanja wa mpira wa Chato kuvutia wawekezaji, watalii
- Serikali imesema hivi karibuni itaanza kujenga uwanja huo katika Wilaya ya Chato ili kuvutia wawekezaji na watalii.
- Pia uwanja wa ndege wa Chato kuwa wa kimataifa.
Dar es Salaam. Katika kuhakikisha Tanzania inafaidika na fursa za utalii katika mikoa ya kanda ya Ziwa Victoria, Serikali imesema itajenga uwanja wa mpira wa Chato ambao utatumika kuvutia wawekezaji na watalii kutembelea maeneo hayo.
Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani aliyekua akizungumza leo (Julai 9, 2019) wakati wa uzinduzi wa hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato iliyopo Wilaya ya Chato mkoani Geita, amesema uwanja huo utakuwa wa kisasa utahamasisha kwa kiasi kikubwa uwekezaji na utalii katika maeneo hayo.
“Hivi karibuni tunajenga uwanja wa mpira wa ‘Chato stadium’ ambao utatumika sana katika kuhamasisha wawekezaji na hasa watalii wanaotoka nje ya nchi yetu,” amesema Dk Kalemani.
Amesema Chato inapakana na Ziwa Victoria, na inachukua eneo kubwa lakini wilaya hiyo ina madini ya kuvutia wawekezaji ambapo Serikali inatengeneza mazingira mazuri kwa ajili yao ikiwemo ujenzi wa mradi wa umeme wa maji wa megawati 2,115 katika mto Rufiji mkoani Pwani.
“Umeme utakuwa wa uhakika, maeneo yote ya nchi yetu lakini hata hapa Chato. Nichukue nafasi hii kuwahakikishia wawekezaji wa ndani na nje ili waje kuwekeza Chato ili nayo baada ya miaka kadhaa itamkike kati ya majiji makubwa hapa chini,” amesema.
Zinazohusiana:
- Tanzania yaangazia masoko 18 duniani kukuza utalii
- Tanzania yang’ara tena tuzo za eneo bora la utalii duniani
- Jiandae kufanya utalii katika hifadhi mpya ya Chato
Hifadhi hiyo mpya iko katika eneo muhimu la kukuza soko la watalii kutoka ukanda wa Magharibi na Mashariki ambapo uwanja wa ndege wa Chato na reli ya kisasa (Standard Gauge Railway) vitakuwa muhimu katika kutoa mawasiliano na usafiri wa uhakika.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamis Kigwangalla amesema hifadhi ya Taifa ya Burigi Chato ina mvuto wa kipekee na pengine ni hifadhi ya kipekee zaidi Afrika kwa ukubwa ambapo itakuwa hifadhi ya tatu nchini ikitanguliwa na Ruaha na Serengeti.
Amesema ili kuhakikisha hifadhi hiyo inapata msukumo wa aina yake na kukuza utalii katika kanda ya ziwa, uboreshaji wa miundombinu unafanyika ikiwemo ujenzi wa hoteli na barabara kwa ajili ya mizunguko katika hifadhi.
“Mhe. Rais haujawekeza katika hifadhi pekee bali umejenga miundombinu, tulikushauri uufanye uwanja wa ndege wa Chato kuwa uwanja wa kimataifa na tunashukuru umeridhia, kwa hiyo uwanja wa ndege wa Chato hautokuwa wa kawaida kama uwanja wa ndege wa Tabora au Musoma,” amesema Dk Kigwangalla.
Uwekezaji unaohitajika katika eneo hilo ni ujenzi wa hoteli zenye hadhi ya nyota moja hadi zenye nyota tano, nyumba za kulala wageni, uanzishwaji wa kampuni za utalii pamoja na kutoa huduma za vyakula kwa ajili ya watalii.
Tayari Serikali imefuta kodi ya kuingiza magari ya watalii nchini ili kuwawezesha wananchi na wawekezaji kuingia katika biashara hiyo ikiwa na lengo la kuongeza mapato ya Serikali kupitia sekta ya utalii.