Sababu za Serikali kuziunganisha benki za TPB, TIB Corporate
- Msajili wa hazina asema uamuzi huo umelenga kuboresha utendaji wa benki inazozimiliki ili kuwa na benki moja ya biashara ambayo ni imara.
- Kwa hatua za awali TPB Bank PLC itachukua mali na madeni yote ya TIB Corporate.
- TIB Corporate ni benki ya tatu ya umma kuunganishwa na TPB Bank PLC ndani ya miaka mitatu iliyopita.
Dar es Salaam. Serikali ya Tanzania imeziunganisha benki ya TPB Bank PLC na TIB Corporate ikibainisha kuwa uamuzi huo umelenga kuboresha utendaji wa benki inazozimiliki.
TIB Corporate ni benki ya tatu ya umma kuunganishwa na TPB Bank PLC ndani ya miaka mitatu iliyopita jambo ambalo linazidi kuiongezea nguvu benki ya TPB sokoni.
Msajili wa Hazina Athumani Mbuttuka ameeleza katika taarifa kwa umma kuwa uunganishaji wa benki hizo unaanza Jumatatu, Juni Mosi na kwamba kwa hatua za awali TPB Bank PLC itachukua mali na madeni yote ya TIB Corporate.
“Seikali imechukua uamuzi huu kwa lengo la kuboresha utendaji wa benki inazozimiliki ili kuwa na benki moja ya biashara ambayo ni imara,” amesema Mbuttuka.
“Aidha, muungano huu unalenga kuleta mageuzi makubwa ya kiutendaji, kimfumo, kimuundo na kitaswira ili benki hii iweze kuhimili ushindani wa kibiashara kwenye sekta ya fedha,” ameongeza bosi huyo.
Hata hivyo, Mbuttuka hakuweka bayana thamani ya uunganishaji wa benki hiyo wala nguvu ya kifedha ambayo TPB itakuwa nayo baada ya hatua hiyo.
Hii ni mara ya tatu Serikali inaziunganisha benki zake ndani ya miaka mitatu iliyopita. Mara ya kwanza iliziunganisha benki ya Twiga Bancorp na TPB PLC Mei 2018. Miezi mitatu baadaye iliziunganisha Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) na TPB Bank PLC Agosti 2018.
Zinazohusiana:
- NMB yaingiza sokoni huduma tatu za kidijitali kwa mpigo
- BoT yashusha tena riba kwa benki za biashara Tanzania
Mbuttuka amesema wateja wote wa benki za TPB na TIB Corporate wataendelea kuhudumiwa kwenye matawi yao ya sasa hadi hapo wataKapoarifiwa vinginevyo.
“Serikali inawahakikishia wateja wa benki hizi mbili pamoja na umma kuwa huduma za kibenki hazitaathirika kwa vyovyote vile kutokana na mabadiliko haya,” amesema.
Uamuzi wa kuziunganisha benki hizo utafanya benki za biashara Tanzania kubakia 37 kutoka 38 zilizoripotiwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) mapema Januari 2020.
Mbali na benki hizo za biashara, Tanzania ina benki sita za jamii, benki mbili za maendeleo na benki tano za huduma ndogo za kifedha (Microfinance banks).
Latest