Rais Samia, Mkuu mpya wa Majeshi kuteta “inbox”

June 30, 2022 2:24 pm · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Mkuu wa mpya wa Majeshi (CDF), Jacob Mkunda aapishwa Ikulu.
  • Rais Samia aahidi kumpa ushirikiano.
  • Jenerali Mabeyo kuteuliwa katika kazi nyingine.

Dar es Salaam. Rais Samia ameahidi kutoa ushirikiano kwa Mkuu wa mpya wa Majeshi (CDF), Jacob Mkunda na kuhusu maelekezo ya kikazi watazungumza “inbox”.

Jenerali Mkunda aliyeteuliwa jana anachukua nafasi ya Jenerali Venance Mabeyo ambaye amestaafu leo huku Rais Samia akiahidi kumteua katika nafasi nyingine kuendelea kulitumikia Taifa.

Rais Samia aliyekuwa akizungumza leo Juni 30, 2020 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati akimuapisha Jenerali Mkunda amempongeza pamoja na viongozi wengine aliowateua huku akiwataka kuendeleza kazi nzuri aliyofanya Jenerali Mabeyo.

“Kwa wale niliowateua, nawapongeza na kuwatakia kazi njema, mkaanze pale Jenerali Mabeyo alipoishia. Najua kwenye Jeshi hakuna mtu kuingia na yake, ukifika unaanzia alipoachia mwenzio. Nawataka mkafanye kazi kama aliyetoka alivyofanya,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema kuhusu mambo mengine kwa aliwaowateua akiwemo Jenerali Mkunda “maelekezo zaidi tutazungumza inbox.”

Jenerali Mabeyo kupata kazi mpya

Rais Samia amesema Jenerali Mabeyo amestaafu akiwa kijana na bado ana nguvu na sifa za kuendelea kuteuliwa katika nyadhifa mbalimbali.

“Umemaliza utumishi wako ukiwa bado una nguvu hivyo nitaendelea kukuteua na kukupa majukumu uendelee kusaidia kulitumikia Taifa lako. Nadhani jioni ya leo tutakusikia kwenye bomba, Katibu Mkuu atakuwa amekwisha kupangia majukumu,” amesema Rais Samia.

Kiongozi huyo mkuu wa nchi amesema anamshukuru kwa kumjaalia Jenerali Mabeyo kumaliza utumishi wake akiwa bado ana nguvu na kwa kazi nzuri uliyoifanya katika utumishi wake kwani amefanya kazi yake kwa uadilifu mkubwa na umetumikia cheo chake kwa jitihada kubwa.

Kabla ya uteuzi huo, Jenerali Mkunda alikuwa Mkuu wa Tawi la Operesheni na Mafunzo katika Makao Makuu ya Jeshi.

Rais Samia jana pia alimpandisha cheo Meja Jenerali Salum Haji Othman kuwa Luteni Jenerali na alimteua kuwa Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania.

Kabla ya uteuzi huo Meja Jenereali Othman alikuwa Kamishna wa Utafiti na Maendeleo Jeshini katika Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Pia alimteua Luteni Jenerali Mathew Edward Mkingule kuwa Balozi ambapo kabla ya uteuzi huo alikuwa Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

Wateule hao wote wameapishwa leo Ikulu jijini Dar es Salaam.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW