Mwelekeo mpya uzalishaji mali kwenye majeshi ya Tanzania
- Itaongeza bajeti kuyawezesha kutimiza majukumu ya msingi.
- Masharika ya kuzalisha mali kwa kila jeshi kuanzishwa.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amesema Serikali itaongeza bajeti inayoelekezwa kwa majeshi ya Tanzania ikiwemo Magereza kwa mwaka wa fedha wa 2022/23 ili yajielekeze kutimiza majukumu yao ya msingi kuliko uzalishaji mali.
Kwa mujibu wa kiongozi huyo mkuu wa nchi, majeshi hayo (Magereza, Polisi Tanzania, Jeshi la Kujenga Taifa na Jeshi la Wananchi) kwa sasa yamekuwa yakifanya kazi za uzalishaji mali ambzo zinaweza kuyatoa katika majukumu ya kuanzishwa kwao.
“Kwa mwaka ujao wa fedha tumeamua Serikali kuongeza fedha nyingi ndani ya vikosi vyetu ili wajielekeze zaidi sasa kwenda kwenye kazi zao zinazohusu zaidi kuliko uzalishaji mali,” amesema Rais Samia.
Rais Samia aliyekuwa akizungumza leo Machi 25, 2022 wakati akiweka mawe ya msingi kwenye miradi ya Jeshi la Magereza mkoani Dodoma amesema suala la kuzalisha mali haliepukiki ndani ya majeshi hayo lakini inatakiwa kutafuta namna nzuri ya utekelezaji ili kutokuathiri shughuli za msingi.
Rais Samia amependekeza majeshi hayo kuunda mashirika yao yatakayofanya kazi na sekta binafsi kuzalisha mali kuliko kujihusisha moja kwa moja katika shughuli hizo.
“Suala la uzalishaji mali haliepukiki na hapa ndipo nataka niungane na Mheshimiwa Waziri kwamba tuna rasimali nyingi ndani ya majeshi yetu lakini hatuzitumii ipasavyo kwa sababu hatuna uwezo wa kuzitumia.
“Kama tutajipanga vizuri, kila jeshi likawa na shirika lake. Mashirika haya yakapewa watalaam wanaoweza kuyaendesha kibiashara, wakasimamia biashara za majeshi yao, wakaingia mikataba na sekta binafsi, wakaweza,” amesema Rais.
Amesema utaratibu huo umekuwa ukitumika na majeshi mbalimbali duniani na hivyo wakuu wa majeshi hayo wanaweza kwenda kujifunza ili kupata uzoefu wa namna wanavyoweza kutekeleza katika maeneo yao.
“Na zoezi hili hatulianzi sisi, huko ulimwenguni yanafanyika na yapo majeshi yanpata fedha zao kupitia mtindo kama huo. Kwa hiyo niwatake viongozi wa majeshi yetu kwenda kujifunza kwa wenzetu duniani wanaendesha majeshi yao bila kuacha kazi zao za msingi,” amesisitiza Rais.
Latest