Rais Samia kushiriki mkutano AU, Tanzania ikimaliza muda wake Baraza la Amani 

February 12, 2026 3:26 pm · Kelvin Makwinya
Share
Tweet
Copy Link
  • Mkutano unatarajia kujadili mustakabali wa rasilimali maji, afya ya jamii na maendeleo endelevu barani Afrika.
  • Rais Samia pia anatarajia kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali wa Afrika na taasisi za kimataifa  kuimarisha ushirikiano wa kisiasa, kiuchumi na kimaendeleo.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameondoka nchini leo Februari 12, 2026 kuelekea Addis Ababa, Ethiopia, kushiriki Mkutano wa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU), kujadili mustakabali wa rasilimali maji, afya ya jamii na maendeleo endelevu katika bara.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu, mkutano huo unatarajiwa kufunguliwa rasmi Februari 14, 2026, ukiwa na kaulimbiu isemayo “Kuhakikisha Upatikanaji Endelevu wa Maji na Huduma Salama za Usafi wa Mazingira ili Kufikia Malengo ya Agenda 2063.” 

“Kaulimbiu hiyo inalenga kuhimiza hatua za pamoja za bara katika kuhakikisha usalama wa rasilimali maji, afya ya jamii, na maendeleo endelevu,” imeeleza taarifa hiyo.

Mkutano unatarajia kujadili mustakabali wa rasilimali maji, afya ya jamii na maendeleo endelevu barani Afrika. Picha | Ikulu Mawasiliano.

Aidha, kabla ya mkutano huo Rais Samia anatarajiwa kuhiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC) utakaofanyika Februari 13, 2026 chini ya uenyekiti wa Rais wa Kenya, William Ruto kujadili masuala mbalimbali yanayohusu tabianchi suala linaloendelea kuathiri upatikanaji wa maji, uzalishaji wa chakula na ustawi wa jamii.

Tanzania kumaliza muda wake Baraza la Amani 

Mbali na kujadili masula hayo, katika mkutano huo pia Tanzania inatarajia kukamilisha rasmi kipindi chake cha kuhudumu katika Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika baada ya kulitumikia kwa vipindi viwili mfululizo kuanzia mwaka 2022 hadi 2026 na kutoa mchango mkubwa katika kuimarisha amani, utulivu na usalama barani Afrika.

Aidha, kwa mwaka 2026 uongozi wa AU unatarajiwa kukabidhiwa rasmi kwa nchi ya Burundi, huku Tanzania ikiteuliwa kuwa Makamu wa Pili wa Mwenyekiti, kuwakilisha Kanda ya Mashariki, hatua inayotajwa kuendelea kuipa Tanzania nafasi ya kuchangia maamuzi na mwelekeo wa Bara la Afrika.

Rais Samia pia anatarajia kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali wa Afrika na taasisi za kimataifa  kuimarisha ushirikiano wa kisiasa, kiuchumi na kimaendeleo. Picha | Ikulu Mawasiliano

Katika hatua inayotajwa kuipa Tanzania ushawishi katika ajenda za kijamii barani Afrika, Rais Samia amependekezwa kuteuliwa kuwa Kinara wa Umoja wa Afrika katika masuala ya Afya ya Mama na Mtoto, uteuzi unaotarajiwa kupitishwa rasmi katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu, mbali na kushiriki mkutano huo, Rais Samia pia anatarajiwa kufanya mazungumzo ya pande mbili na viongozi mbalimbali wa Afrika na taasisi za kimataifa, akiwemo Waziri Mkuu wa Ufalme wa Eswatini, Russell Dlamini, Rais wa Umoja wa Visiwa vya Comoro, Azali Assoumani, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Amina Mohammed, pamoja na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Dk Sidi Ould Tah, kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kisiasa, kiuchumi na kimaendeleo.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks