Rais Samia amlilia Jenerali Msuguri
- Amefariki akiwa na miaka 104 wakati akipatiwa matibabu mkoani Mwanza
- Atakumbukwa kwa kuongoza majeshi ya Tanzania kwenye vita dhidi ya Idd Amin Dada
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ametoa salamu za pole kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Jacob John Mkunda, Makamanda, wapiganaji wastaafu, wanafamilia na Watanzania kutokana na kifo cha Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Mstaafu Jenerali David Bugozi Musuguri.
Kwa mujibu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) Mkuu wa Majeshi Mstaafu, Jenerali David Musuguri, amefariki Dunia leo, Oktoba 29, 2024, jijini Mwanza alipokuwa akipatiwa matibabu.
Jenerali Musuguri, aliyezaliwa Januari 4, 1920 huko Butiama Mkoani Mara ameitumikia JWTZ kuanzia Mwaka 1942 hadi 1988 akihitimisha Uongozi wake kama Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi kati ya 1980 na 1988 ambapo alianza kazi yake kijeshi katika Jeshi la King’s African Rifles (KR) na Tanganyika Rifles kabla ya kujiunga na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Jenerali Musuguri atakumbukwa zaidi kwa kuongoza majeshi ya Tanzania katika vita dhidi ya Idi Amin Dada wa Uganda Mwaka 1978, baada ya uvamizi wa eneo la Kyaka, Mkoani Kagera.
JWTZ imebainisha mapambano na vita nyingine alizoshiriki ni pamoja na Vita Kuu ya Pili ya Dunia, Battle of Madagascar, Vita vya Kagera, na Battle of Simba Hills.
Katika Salamu zake za pole Rais Samia amesema Jenerali Musuguri ameitumikia nchi kwa weledi, umahiri, kujituma, ushujaa, nidhamu na kwa mafanikio ya hali ya juu, akiishi kiapo chake cha kuwa tayari kuutoa uhai wake ajili ya ulinzi wa Taifa letu.
“Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa zawadi ya maisha yake ya miaka 104, ambapo miaka 46 kati ya hiyo ameitumikia nchi yetu kwa weledi, umahiri, kujituma, ushujaa, nidhamu na kwa mafanikio ya hali ya juu, akiishi kiapo chake cha kuwa tayari kuutoa uhai wake ajili ya ulinzi wa Taifa letu.
Ametuachia mfano bora wa utumishi wa umma utakaoendelea kuwa mwanga ndani na nje ya Majeshi yetu. Mwenyezi Mungu ailaze roho yake mahali pema peponi. Amina,” amesema Rais Samia.
Latest
