Rais Samia ahaidi Sh1 bilioni Taifa star ikibeba ubigwa CHAN 2024
- Iwapo Taifa stars itafika hatua ya fainali, itapewa Sh500 milioni
- Nusu fainali Sh200 milioni na goli la mama Sh20 milioni.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameahidi zawadi ya Sh1 bilioni kwa wachezaji na benchi la ufundi la timu ya Taifa (Taifa Stars) endapo watafanikiwa kutwaa ubingwa wa michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (CHAN) 2024.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Prof Palamagamba Kabudi, aliyekuwa akizungumza na waandishi wa habari leo Julai 24, 2024 katika uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam, amesema ahadi hiyo ni sehemu ya kuongeza hamasa kwa wachezaji na kuonyesha imani ya Serikali kwa uwezo wao.
“Katika kuhamasisha ushindani na uzalendo, Mheshimiwa Rais ameahidi kuwazawadia vijana wetu Sh1 bilioni endapo watafanikiwa kutwaa ubingwa wa CHAN 2024. Kauli mbiu ni moja mcheza kwao hutuzwa,” amesema Prof. Kabudi.
Ahadi hiyo ya Rais Samia kwa wachezaji wa timu ya Taifa ya Tanzania inakuja ikiwa zimesalia siku nane kuanza kwa michuano hiyo Agosti2, mwaka huu.
Awali, michuano hiyo ilipangwa kufanyika kuanzia Februari mosi hadi 28 mwaka 2025 huku mechi za kufuzu zikichezwa kati ya Oktoba na Disemba mwaka 2024, kabla haijaahirishwa Januari 14 ,2024 ni siku 18 tu kabla ya kuanza kwake.
Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), hairisho hilo limesababishwa wataalamu kushauri lisogezwe mbele ili kuhakikisha miundombinu na vifaa vya fainali hizo viko katika viwango vinavyohitajika.
Kabudi aliwaambia wanahabari kuwa iwapo Taifa stars itafika hatua ya fainali, itapewa Sh500 milioni, nusu fainali Sh200 milioni na Sh20 milioni wa kila goli litakalofungwa katika mashindano hayo.
Kwa mujibu wa Prof Kabudi, maandalizi yote muhimu yamekamilika ambapo ni pamoja na malipo ya ada za ushiriki, ukarabati wa viwanja vya mechi na mazoezi, pamoja na uundaji wa kamati mbalimbali za uratibu.
Pia, Kabudi amethibitisha kuwa viwanja vya Benjamin Mkapa na Azam Complex tayari vimepata kibali rasmi kutoka kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF) baada ya ukaguzi wa kitaalamu.
Michuano hii ya CHAN, inayojulikana kwa jina la PAMOJA CHAN 2024, itaandaliwa kwa ushirikiano kati ya Tanzania, Kenya na Uganda, kuanzia Agosti 2 hadi Agosti 30, 2025.
Tanzania kuwa mwenyeji wa makundi wawili
Tanzania imepewa heshima ya kuandaa makundi mawili kati ya manne ya mashindano.
Kundi B litacheza jijini Dar es Salaam likihusisha timu za Tanzania, Burkina Faso, Mauritania, Jamhuri ya Afrika ya Kati, na Madagascar.
Kundi D litacheza visiwani Zanzibar katika uwanja wa Amaan, likijumuisha Nigeria, Senegal, Sudan na Congo.

Aidha, Waziri huyo ameeleza kuwa nchi imepewa hadhi ya kuandaa mechi ya ufunguzi kati ya Taifa Stars na Burkina Faso, itakayochezwa Agosti 2, 2025 saa 2 usiku katika Uwanja wa Benjamin Mkapa ambapo mgeni rasmi kwenye sherehe za uzinduzi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Prof Kabudi, ameeleza kuwa Serikali imeweka viingilio vya bei nafuu ili kuwawezesha mashabiki wengi kushiriki, Sh2,000 kwa mzunguko, Sh5,000 kwa VIP B na Sh10,000 kwa VIP A.
Kwa upande wake, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, amehimiza ushirikiano wa vyombo vya habari, wasanii, na mashabiki katika kampeni ya kitaifa ya kuunga mkono timu ya taifa kuelekea CHAN 2024.