Rais Samia aagiza maboresho sheria ya uwekezaji Tanzania
- Ataka kipengele cha utatuzi wa migogo kiangaliwe upya.
- Asema itasaidia kuwalinda wawekezaji wanaokuja nchini.
- Mawakili watakiwa kuwa walinzi wa uwekezaji nchini.
Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan ameagiza kufanyika kwa mabadiliko ya sheria za utatuzi wa migogoro baina ya Serikali na wawekezaji ili kuimarisha sekta hiyo nchini.
Rais Samia aliyekuwa akifungua mkutano mkuu wa Chama Cha Mawakili wa Serikali jijini Dodoma leo Septemba 29, 2022 amesema sheria hiyo imekuwa ikichangia kuwaondoa wawekezaji nchini kwa sababu baadhi ya vipengele vyake vina changamoto katika utatuzi wa migogoro.
Sheria hiyo (Tanzania Investment Act) iliyokuwepo kwa muda mrefu nchini inamtaka muwekezaji kutumia sheria zilizopo nchini kutatua migogoro itakayoibuka wakati wa uwekezaji, jambo ambalo baadhi ya wawekezaji hawakubaliani nalo.
“Kama mtu anakuja na pesa yake kubwa anaiwekeza ndani ya nchi, mzozo unapotokea mimi nitakuhukumu…wengine wanatukimbia kwa sababu hiyo,” amesema Rais Samia.
Mabadiliko ya sheria ya kulinda uwekezaji yanatakiwa yazingatie uwepo wa shirika au taasisi (mtu wa tatu) itakayosimamia na kutatua mzozo au mgogoro utakaoibuka wakati wowote kipindi cha muda wa uwekezaji.
“Kuna mashauri ambayo kweli tunayaweza kuyafanya hapa ndani lakini kuna mashauri ambayo muwekezaji aliyesreious (makini) ukimpa haji anakimbia,” amesema Samia.
‘Uwekezaji lazima ulindwe’
Rais Samia akiwa kwenye mkutano huo amesisitiza wanasheria kulinda uwekezaji wowote unaofanyika nchini ili kuweza kupokea wawekezaji wengi zaidi, kukuza mapato na uchumi wa nchi.
“Mnaweza kujiuliza mimi wakili wa Serikali nahusika nini kwenye kukuza uchumi?, nyinyi ndiyo majeshi wa kulinda uwekezaji wetu, ni walinzi wa kalamu na siyo wa bunduki,” ameongeza Rais.
Soma zaidi
-
Nchi 5 zinazoongoza kwa maambukizi ya Uviko-19 Afrika
-
Kwa nini mchango wa sekta ya misitu ni mdogo katika pato la Taifa?
Sambamba na hilo ametaka mikataba yote ya Serikali kusainiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ili kuzuia migogoro isiyo na ulazima inayoibuka kutokana na mikataba inayosainiwa bila utaratibu.
“Kuna mikataba watu wanajiingilia tu huko alafu inapoleta mzozo ndiyo wanarudi kwa AG tusaidie…pengine aliyeingia mkataba huo hayupo au alishakufa,” amesema Rais.
Sheria zibadilishwe
Awali kwenye mkutano huo Jaji Mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Juma ametaka mabadiliko mbalimbali yafanyike kwenye sheria zilizopo nchini ili kuleta matokeo chanya kwenye kitengo cha sheria na nchi.
“Tunatakiwa kubadilisha maudhui ya sheria zetu zitumie teknolojia zitakazowawezesha kufanya maamuzi kwa haraka…wenzetu wanatumia kompyuta kwa hiyo hatuwezi kushindana nao kwenye eneo la biashara,” amesema Jaji Mkuu.
Aidha, Prof Juma ameeleza umuhimu wa kitengo cha sheria kushiriki kwenye maboresho ya sekta ya elimu yanayofanyika na wadau wa elimu kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili kutengeneza mazingira mazuri kwa wanasheria wanaokuja.
“Wanasheria inabidi tuwe sehemu ya mabadiliko ya elimu kwa sababu ule ndiyo msingi au chemchemi ya wanasheria wanaokuja,” amesema Jaji Mkuu.