Rais Magufuli awajia juu TRA, awataka wabuni vyanzo vipya vya kodi

Rais John Magufuli akimuapisha Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka Mapato Tanzania (TRA) Msafiri Mbibo leo Ikulu jijini Dar es Salaam. Picha|Michuzi blog.
- Amesema haridhishwi na utendaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukusanyaji wa kodi na kuitaka mamlaka hiyo kutanua wigo wa walipa kodi kwa kubuni vyanzo vipya vya kodi na kujenga mazingira rafiki ya watu wengi kulipa kodi.
- Ameeleza kutofurahishwa na mrundikano wa kesi za kodi mahakamani na ametaka tatizo hilo lifanyiwe kazi na mamlaka husika.
Dar es Salaam. Rais John Magufuli amesema haridhishwi na utendaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika ukusanyaji wa kodi na kuitaka mamlaka hiyo kutanua wigo wa walipa kodi kwa kubuni vyanzo vipya vya kodi na kujenga mazingira rafiki ya watu wengi kulipa kodi.
Rais Magufuli aliyekuwa akizungumza leo (Aprili 1, 2019) Ikulu jijini Dar es Salaam mara baada ya kumuapisha Naibu Katibu Mkuu wa Wizara Fedha na Mipango atakayeshughulikia sera, Adolf Ndunguru na Naibu Kamishna Mkuu wa Mamlaka Mapato Tanzania (TRA) Msafiri Mbibo amesema mpaka sasa walipa kodi wanaotambulika rasmi na TRA ni 2.7 milioni tu kati ya watanzania zaidi ya 55 milioni ambapo inawaumiza walipa kodi wachache kwa kuwapangia viwango vikubwa vya kodi.
Amesema TRA ina uwezo wa kupanua wigo wa ulipaji kodi kwa kuweka viwango vya kodi vitakavyowavutia walipa kodi wengi lakini imeshindwa badala yake inawakamua walipa kodi wachache.
“Ukienda mipakani wafanyabiashara wanafungua maduka upande nchi za wenzetu na siyo upande wa Tanzania, na sababu kubwa ni kwamba wakifungua upande wa Tanzania wanasumbuliwa na TRA, wekeni viwango vya kodi vinavyolipika ili watu wengi waweze kulipa kodi badala ya kukwepa” amesisitiza Rais.
Amesema TRA wanapaswa kubuni vyanzo vipya vya kodi na kuhakikisha wanatengeneza mazingira mazuri yatakayovutia watu wengi kulipa kodi.
Soma zaidi:
Hata hivyo, ameeleza kutofurahishwa na mrundikano wa kesi za kodi mahakamani na ametaka tatizo hilo lifanyiwe kazi kwa kuwa linasababisha kodi nyingi kutolipwa kwa kusubiri mivutano ya kesi na kuwataka Mbibo na Ndunguru kurekebisha dosari zilizopo katika ofisi zao ikiwa ni pamoja na kuwaondoa watumishi wanaoonekana ni kikwazo cha kutekeleza mipango yao.
Hafla ya kuapishwa kwa viongozi hao imehudhuriwa na Makamu wa Rais Sarnia Suluhu Hassan, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi, Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dk Ashatu Kijaji, Makatibu Wakuu, Viongozi Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama na wafanyakazi wa Wizara ya Fedha na Mipango.
Mama Samia amesema viongozi hao wanatarajiwa kufanya vizuri zaidi katika nafasi walizopewa hivi sasa hasa ikizingatiwa kuwa wanakwenda kufanya kazi katika ofisi zenye mchango mkubwa katika uchumi wa nchi.