Precision Air yasitisha safari za ndege Nairobi
- Ni kutokana na mgomo unaoendelea jijini Nairobi Kenya.
- KCAA yaagiza kurejeshwa kwa usafiri wa anga.
Arusha.Shirika la Ndege la Precision Air limetangaza kusitisha safari zake zote za kuingia na kutoka jiji la Nairobi kufuatia mgomo wa Chama cha Wafanyakazi wa Usafiri wa Anga nchini Kenya (KAWU).
Mgomo huo unaoshuhudiwa kwa siku ya pili katika uwanja wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) ambao ni miongoni wa mwa viwanja vyenye shughuli nyingi zaidi barani Afrika umesababisha mamia ya abiria kukosa usafiri huo muhimu.
Taarifa ya Precision Air iliyotolewa leo Februari 17, 2026 imetangaza kusitishwa kwa shughuli zote za usafiri siku ya leo ikiwaomba radhi abiria wanaotumia shirika hilo.
“Tunaomba radhi kwa usumbufu wowote unaoweza kujitokeza. Kwa abiria walioathirika, timu yetu inafanya kazi kwa haraka kupanga chaguo mbadala la safari.
…Tunaendelea kufuatilia hali hii kwa karibu na tutatoa taarifa zaidi kadiri itakavyopatikana,” imesema taarifa ya Precision Air iliyochapishwa katika ukurasa wa Instagram.

Baadhi ya abiria waliokwama katika Uwanja wa Ndehe wa Kimataifa Jomo Kenyatta baada ya usafiri wa ndege kusitishwa.Picha /Reuters.
Aidha, Shirika hilo limewashauri abiria kuangalia barua pepe na ujumbe mfupi (SMS) mara kwa mara kwa taarifa mpya, kuepuka kwenda uwanja wa ndege kabla ya kuthibitisha hali ya ndege anayotarajia kupanda pamoja na kuhakikisha mawasiliano yao yamesasishwa (updated).
Pamoja na hayo abiria wametakiwa kuwasiliana na shirika hilo kwa namba za simu +255 746 984 100 / +255 784 108 800 au barua pepe kwa anwani ya contactcentre@precisionairtz.com.
KCAA yaagiza kurejeshwa kwa usafiri wa anga
Mamlaka ya Usafiri wa Anga nchini Kenya (KCAA) imetangaza kufanya mkutano na umoja wa wafanyakazi hao na kuagiza shughuli za usafiri wa anga zirejeshwe mara moja.
Taarifa ya KCAA iliyotolea mchana wa leo inabainisha kuwa tayari viongozi wa Serikali pamoja na viongozi wa chama hicho wamefanya mazungumzo na kukubaliana kurejesha shughuli hizo mara moja.
“Pande zote zilikubali rasmi kurejea kazini mara moja. “Usafiri wa anga unachangia pakubwa katika uchumi wa nchi na tumejitolea kuhakikisha kuwa sekta hii inabakia kuwa tulivu,” imesema taarifa hiyo ikimnukuu Katibu wa Baraza la Mawaziri wa Kenya Davies Chirchir.
Latest