NMB Bank yatangaza gawio la Sh610 kwa hisa 2025
- Ni sawa na ongezeko la asilimia 42.2 kutoka gawio la Sh428.85 kwa kila hisa mwaka 2024.
- Gawio hilo ni sawa na asilimia 4.7 ya thamani ya hisa moja kwa bei ya Mei 19, 2026.
Dar es Salaam. Benki ya NMB imependekeza gawio la Sh610.15 kwa kila hisa kwa mwaka 2025 sawa na ongezeko la Sh181.3 kutoka gawio lililotolewa mwaka 2024, ikiwa ni miezi miwili tu baada ya kutangaza faida ya kihistoria.
Katika pendekezo hilo, Bodi ya Wakurugenzi ya NMB imependekeza gawio la kawaida la Sh504.26 pamoja na gawio maalum la Sh105.89 kwa kila hisa.
Kwa pamoja, kiwango hicho pendekezwa ni ongezeko la asilimia 42.2 kutoka gawio la Sh428.85 kwa kila hisa la mwaka 2024.
Kwa mujibu wa taarifa ya NMB malipo hayo ya gawio kwa wanahisa yanatokana na kiasi cha Sh305.08 bilioni kilichotengwa kutoka katika faida baada ya kodi cha Sh756 bilioni iliyopatikana mwaka 2025.

Iwapo gawio hilo litapitishwa na mkutano mkuu wa wanahisa wa benki hiyo utakaofanyika Juni 10, 2026 jijini Dar es Salaam, litaanza kulipwa kuanzia Juni 24, 2026.
Hii ni mara ya tatu mfululizo gawio la benki hiyo ya kibiashara yenye hisa ghali zaidi katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) linaongezeka, fursa inayowapa wawekezaji wake marejesho ya uwekezaji wao. Hadi soko linafungwa jana jioni Mei 19, 2026 hisa moja ya NMB ilikuwa inauzwa kwa Sh13,120.
Ongezeko hilo la gawio ni vigelegele kwa wawekezaji ambao wataendelea kutunisha mifuko kutokana uwekezaji wao kwenye benki hiyo iliyokua kwa kasi zaidi ndani ya miaka 10.
Hivi karibuni pia NMB iliweka kibindoni Dola za Marekani 180 milioni (takriban Sh463.5 bilioni ) kutoka katika taasisi za kimitaifa za kifedha kama mkopo na uwekezaji kwa ajili ya kupanua utoaji wa mikopo nafuu ya ya muda mrefu wakulima pamoja na wafanyabiashara wadogo na wakati (SMEs).
Latest