Ndugai kuzikwa Kongwa Agosti 11, 2025
- Ni baaada ya ibada ya kuagwa itakayofanyika katika viwanja vya Bunge Agosti 10, 2025 jijini Dodoma.
Dar es Salaam. Aliyekuwa Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai, anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumatatu, Agosti 11, 2025 nyumbani kwake Kongwa, mkoani Dodoma.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Spika wa Bunge la Tanzania, Dk. Tulia Ackson, wakati akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwa marehemu jijini Dodoma, shughuli za kumuaga kitaifa zitafanyika siku ya Jumapili, Agosti 10, 2025 asubuhi katika viwanja vya Bunge.
Tulia amesema siku ya Jumatatu, Agosti 11, mwili wa marehemu utasafirishwa kuelekea nyumbani kwake Kongwa kwa ajili ya kupumzishwa.
Ndugai alifariki dunia Agosti 6, 2025 jijini Dodoma akiwa na umri wa miaka 62. Hata hivyo, chanzo cha kifo chake hakijawekwa wazi na familia pamoja na viongozi wa Bunge.
Ndugai alizaliwa Januari 22, 1963, na alikuwa Mbunge wa Jimbo la Kongwa kwa miaka kadhaa kabla ya kuchaguliwa kuwa Naibu Spika mwaka 2010.
Baadaye alihudumu kama Spika wa Bunge kuanzia mwaka 2015 hadi alipojiuzulu Januari 2022.
Hata hivyo, Spika Tulia amesema marehemu Ndugai alikuwa kiongozi mwenye msimamo imara katika masuala mbalimbali, jambo alilojifunza na kulithamini.
“Ni sehemu ya kiongozi kuwa na msimamo, kwa hiyo nilijifunza kuwa na misimamo na kusimamia jambo,” amesema Dk.Tulia.