Watu 22 wafariki dunia baada ya kufukiwa na kifusi Simiyu
- Wafukiwa na kifusi katika mgodi haramu uliogunduliwa wiki tatu zilizopita baada ya kunyesha mvua kubwa.
Dar es Salaam. Watu 22 wamefariki dunia baada ya kufukiwa na kifusi katika mgodi usio rasmi wa dhahabu mkoani Simiyu kufuatia mvua kubwa ilionyesha usiku wa kuamkia Jumamosi.
Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Simon Simalenga amesema kuwa watu hao walikuwa wakifanya uchimbaji katika eneo jipya lililogunduliwa madini hayo wiki mbili au tatu zilizopita.
Simalenga amesema kuwa awali walielezwa kuwa watu kati ya 19 hadi 20 walikuwa wamefukiwa na kifusi hicho katika ajali iliyotokea mapema Jumamosi hii.
“Hata hivyo, wakati wa ukoaji bahati mbaya tumeokoa miili 22 hadi sasa na zoezi la utafutaji na uokoaji linaendelea na mpaka sasa tupo asilimia 98, naweza kusema tupo katika hatua za mwisho kabisa za ukoaji,” Simalenga ameeleza kwa njia ya simu na kuongeza kuwa wanachambua kifusi hicho kuhakikisha wanaokoa watu wote.
Mkuu huyo wa wilaya amesema kundi kubwa la vijana kutoka pande mbalimbali za kanda ya ziwa wenye miaka kati ya 24 na 38 walivamia eneo jipya lililogunduliwa dhahabu na kuanza shughuli za uchimbaji bila kupatiwa kibali na Serikali.
Wachimbaji wadogo wa dhahabu katika mgodi wa Chitongo wilayani Misungwi wakiendelea na shughuli ya kupiga rora ili kuvuta mfuko wa mchanga wa dhahabu ambao unachimbwa ndani ya shimo. Migodi midogo hutumia mbinu na zana ambazo haendani na taratibu za kiusalama. Picha | Mariam John/Nukta Africa.
Afisa mkazi wa madini wa mkoa wa Simiyu, kwa mujibu wa Simalenga, alienda kuwazuia kuchimba mpaka taratibu za uchimbaji kukamilika lakini usiku huo huo vijana hao walirejea na kuendelea kuchimba hadi ajali ilipowafika.
“Mpaka muda navyoongea nawe Waziri wa Madini Antony Mavunde na Katibu Mkuu wa madini tupo mbugani tunaelekea eneo la tukio…kwa makubaliano ya awali kwa maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kwamba Serikali itasimamia taratibu za kuhakikisha miili hiyo inafika kwa familia za wahusika,” amesema Simalenga.
Miaka ya hivi karibuni Serikali ya Tanzania imekuwa ikitoa mafunzo na kusimamia usalama wa migodi ya wachimbaji wadogo wadogo nchini lakini bado baadhi huanzisha migodi hiyo ya madini kinyemela jambo linalotishia usalama wao na mazingira wanayochimba.
Aprili 2015 watu 19 walipoteza maisha mkoani Shinyanga baada ya mgodi haramu wa wachimbaji wadogo kuwafunika na kuwachukua uhai wao.