Mkuu wa Mkoa Mwanza awafunda viongozi wa Chadema
- Awataka kushirikiana kwa pamoja kuleta maendeleo kwa wananchi.
- Asema 4R za Rais Samia zitawasaidia katika kutatua na kusuluhisha migogoro ya wananchi kwa pamoja.
Mwanza.Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Saidi Mtanda amewataka viongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)kuhakikisha wanashirikiana kwa pamoja katika kuwaletea wananchi maendeleo bila kujali vyama vyao.
Mtanda ameyasema hayo leo Mei 1, 2024 ofisini kwake mkoani Mwanza ambapo viongozi wa chama hicho walienda kujitambulisha huku akiwasisitiza kutembea na R nne za Rais Samia Suluhu Hassan ambazo ni Maridhiano (Reconciliation), Mabadiliko (Reforms), Ustahimilivu (Resilience) na Kujenga upya (Rebuilding) katika kutatua na kusuluhisha migogoro ya wananchi kwa pamoja.
“Kwa pamoja tunatakiwa kuwa wastahimilivu na kuvumiliana pale ambapo chama cha upinzani kinapoikosoa Serikali, lazima Serikali iliyopo madarakani iwe na uvumilivu kwa kuwa wanaokosoa hawatoki kwenye familia wala chama kimoja,” amesema Mtanda.
Mtanda amesema kama kiongozi wa mkoa huo yupo tayari kupokea ushauri unaojenga kutoka kwa mtu yeyote.
“Hatuwezi kujenga uchumi wa nchi pasipo kuwa na amani, hivyo tukosoane huku tukijua tunatakiwa kujenga nchi yetu kwa pamoja bila kuangalia vyama vyetu,” amesema Mtanda
Aidha, Mtanda amesema amefurahishwa na kitendo kilichofanywa na viongozi hao kwenda kujitambulisha ofisini kwake na kuwaeleza kuwa yeye ni kiongozi ambaye hapendi kutumia mabavu katika kuongoza na ni mtu ambaye anapenda kumsikiliza kila mtu na anayependa amani.
“Wote sisi ni wazalendo kwa nchi yetu na hatuwezi kuwa chama kimoja, kinachotakiwa ni kukosoana kwa lugha ya staha na kuifanya heshima ya utu wetu, ni dhahiri kwamba ukiwa mkubwa unapenda kuheshimiwa na wadogo pia kwa sababu heshima ni kitu muhimu katika maisha ya watu,” amesema Mtanda
Amewataka viongozi hao kushirikiana pamoja katika kutekeleza na kutatua migogoro ya wananchi.
Mwenyekiti wa Kanda wa Chadema, Ezekiel Wenje amesema chama hicho ni muhimu katika suala la maendeleo kwa nchi hii kwa kuwa maoni wanayotoa yanatakiwa kuisaidia Serikali kutatua changamoto zilizopo.
Amesema hawakosoi tu kwa kuwa wanataka kukosoa bali wanajaribu kuiambia Serikali kufanyia kazi masuala kadha wa kadha ambayo inatakiwa kufanyia kazi na kuipeleka nchi mbele.
“Tunapotoa maoni sio kwamba tunaikosoa Serikali bali tunaiambia ijaribu kupunguza kodi kwani mafuta yakiwa ghali yanaenda kuathiri bei ya vitu vyote katika uchumi,” amesema Wenje.