Miundombinu ya usafirishaji itakavyokuza utalii Kanda ya Ziwa
Naibu waziri wa Utalii, Mary Masanja akizungumza na wananchi baada ya kutembelea ujenzi wa daraja la JPM Kigongo-Busisi. Picha | Mariam John.
- Ni pamoja na daraja la Kigongo-Busisi, reli ya kisasa.
- Itasaidia kuvutia wawekezaji kutembelea vivutio vilivyopo katika mikoa hiyo ya kanda hiyo.
Mwanza. Miradi ya kimkakati inayoendelea kutekelezwa na Serikali mkoani Mwanza inaenda kufungua fursa za utalii katika mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali, amesema Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja.
Masanja ameeleza hayo katika ziara ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipokuwa akikagua maendeleo ya ujenzi wa daraja la Kigongo- Busisi, ujenzi wa reli ya kisasa SGR eneo la Fela na uzinduzi wa jengo la huduma ya macho katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando.
Ametaja miradi ya kimkakati itakayosaidia kukuza utalii kuwa ni ujenzi wa daraja la Kigongo-Busisi, ujenzi wa reli ya kisasa SGR katika eneo la Fela, meli na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Mwanza.
“Tunaamini kanda ya ziwa itakuwa ni kitovu mahususi cha utalii nchini,” amesema Masanja.
Waziri huyo amesema uwepo wa miradi hiyo utarahisisha usafiri kwa watalii wanaotembelea jiji hilo kutoka nchi za jirani na wakati huo huo Wizara inaendelea kupanua wigo wa utalii kupitia utalii wa mikutano na utalii wa majini.
Waziri Masanja amehamasisha wananchi hususan wa Mkoa wa Mwanza kuendelea kupanda miti ili kutunza mazingira, kutunza uwepo wa hali ya hewa nzuri na kutunza vyanzo vya maji.
“Wizara ya Maliasili na Utalii ina mkakati wa kuhakikisha kila mwananchi anapanda miti miwili, hivyo imeanzisha vitalu vya miti ambayo itagawiwa kwa wananchi,” amesema.
Ziara ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa inaendelea mkoani Mwanza ambapo leo Oktoba 17, 2022 atatembelea kisiwa cha Ukerewe, kisiwa cha Gana na kukagua maendeleo ya ujenzi wa stendi ya mabasi ya Nyegezi.