Microsoft mbioni kuingiza sokoni “simu ya Android”
- Inakusudia kuingiza sokoni kifaa kinachofanana na simu janja cha ‘Microsoft Surface duo’ ifikapo 2020.
- Moja ya sifa yake ya pekee ni uwezo wake wa kutumia mfumo endeshi wa Android ambao hautumiki na simu za Microsoft.
Kampuni ya Microsoft ya nchini Marekani inakusudia kuingiza sokoni kifaa kinachofanana na simu janja cha ‘Microsoft Surface duo’ ifikapo 2020 ili kuwapatia wateja wake bidhaa tofauti na walizozizoea.
Kampuni hiyo ya kompyuta na vifaa vya kielektroniki imeeleza kuwa kifaa hicho kinachofanana na simu kitakuwa kinaendeshwa na mfumo endeshi wa Android ambao haujazoeleka na watumiaji wa bidhaa za kampuni hiyo.
Huenda hatua hiyo, ikawapa uchaguzi watumiaji wa simu za Microsoft zinazotumia mfumo wa Windows, kutumia vifaa vyenye muonekano tofauti.
Kifaa hicho, kina sehemu mbili ya kioo zinazoweza kukunjwa katika muonekano tofauti, zitamuwezesha mtumiaji kupiga simu, kupiga picha kwa kamera na kufanya mambo mengine kama siku za kawaida.
EXCLUSIVE: Take a first look at the Microsoft Surface Duo, a new dual-screen Android ‘device.’ https://t.co/H560iQTR8x
pic.twitter.com/S6x7tBxrD0— WIRED (@WIRED) October 2, 2019
Mkurugenzi Mtendaji wa Microsoft, Satya Nadella amesema kampuni yake inajaribu kutengeneza bidhaa mpya tofauti na zilizozoeleka na kuongeza kuwa hiyo inaweza isiwe simu bali kitu kingine.
Lakini wadadisi wa mambo wanasema, inaweza kuwa ni simu lakini Microsoft haitaki kuweka wazi jambo hilo. Kifaa hicho kinatarajiwa kuingia sokoni na kuanza kutumika mwaka 2020.
Zinazohusiana:
- Whatsapp kuachana na baadhi ya simu za iPhone, Android
- Maswali lukuki mfumo mpya wa Harmony OS, Huawei
Mabadiliko huenda yakaleta manufaa makubwa kwa watumiaji wa Microsoft kwani wataweza kupata programu tumishi ambazo hazipatikani kwenye mfumo wa simu za Windows.
Pia inaweza kuifaidisha kampuni hiyo kujitanua kimasoko ili kuwafikia wateja wengi duniani kwa bidhaa bora zinazotumiwa na watu wengi.
Latest
