Mfahamu panya wa Tanzania mtegua mabomu aliyefariki dunia
Septemba 2021, shirika la usaidizi la mifugo la Uingereza (PDSA) lilimtunuku Magawa medali yake ya dhahabu kwa “kujitolea kuokoa maisha katika eneo na uondoaji wa mabomu hatari ya ardhini nchini Cambodia.” Picha| PDSA.
- Ni panya Magawa mwenye asili ya Tanzania aliyefariki mwishoni mwa wiki.
- Alikuwa akisifika kwa umahiri wake wa kugundua na kutegua mabomu na vilipuzi nchini Cambondia.
- Amesaidia kuokoa maelfu ya maisha ya watu.
Dar es Salaam. Panya mwenye asili ya Tanzania aitwaye Magawa aliyetumika kutafuta na kutegua mabomu ya ardhini na vilipuzi nchini Cambodia amefariki dunia mwishoni mwa wiki akiwa na umri wa miaka nane huku akikumbukwa kwa ushujaa wake wa kuokoa maisha ya watu yaliyokuwa hatarini.
Shirika la APOPO la nchini Ubelgiji lililokuwa linamlea Magawa katika taarifa yake iliyotolewa leo katika ukurasa wake wa Instagram limesema panya huyo ameaga dunia akiwa na miaka nane mwishoni mwa wiki.
“Ni kwa moyo wa masikitiko kwamba tunatoa taarifa za kusikitisha kwamba shujaa Magawa aliaga dunia kwa amani wikendi hii,” imeeleza taarifa ya APOPO.
Kwa mujibu wa APOPO, shirika linalotoa mafunzo kwa wanyama ya kuokoa maisha ya watu, Magawa alikuwa na afya nzuri na alitumia muda mwingi wa wiki iliyopita kucheza kwa shauku yake ya kawaida.
Hata hivyo, kuelekea mwishoni mwa wiki alianza kupunguza kasi, kulala zaidi na kuonyesha hamu kidogo ya chakula katika siku zake za mwisho.
Magawa aliyesheherehekea siku yake ya kuzaliwa Novemba 2021 amefika tamati ya maisha katika umri wa uzee wa miaka nane.
Shirika hilo limesema limeguswa na kifo cha panya huyo shujaa na kushukuru kwa kazi nzuri aliyoifanya siku za uhai wake.
Wakati wa kazi yake, Magawa alipata zaidi ya mabomu 100 ya ardhini na vilipuzi vingine, na kumfanya kuwa shujaa wa APOPO aliyefanikiwa zaidi hadi sasa.
Mchango wake umesaidia watu nchini Cambodia kuishi, kufanya kazi na kucheza bila hofu ya kupoteza maisha au viungo vya mwili kutokana na mabaki ya vilipuzi vya migodini na mabomu baada ya kumalizika kwa vita vya kikatili vya wenyewe kwa wenyewe miaka ya 1970 na 1980.
Soma zaidi:
-
Mambo 10 ya kuyafahamu kabla ya kuanza kufuga kasuku
-
Wafahamu tausi ambao Magufuli alimzawadia Rais Kenyatta
Ushujaa wa kutegua mabomu
Magawa alistaafu Juni mwaka 2021 baada ya kuhitimisha kazi yake ya miaka mingi ya kugundua mabomu ya ardhini nchini Cambodia.
Magawa, aliyekuwa na asili ya Tanzania, amekuwa panya aliyefanikiwa zaidi kufunzwa na kusimamiwa na APOPO kunusa mabomu ya ardhini na kutoa tahadhari kwa wachimbaji ili waweze kuondoa vilipuzi kwa usalama.
Kwa mujibu wa APOPO, Magawa alisaidia kuondoa migodi kutoka eneo la mita za mraba 225,000 (futi za mraba milioni 2.4).
Kifo cha Magawa huenda siyo cha bahati mbaya kwa sababu kwa wastani wa maisha ya panya mkubwa wa Kiafrika ni miaka nane.
Panya Magawa akiwa katika mafunzo ya kutegua mabomu kabla hajafariki dunia. Picha| PDSA UK.Panya aliyeshinda tuzo
Septemba 2021, shirika la usaidizi la mifugo la Uingereza (PDSA) lilimtunuku Magawa medali yake ya dhahabu kwa “kujitolea kuokoa maisha katika eneo na uondoaji wa mabomu hatari ya ardhini nchini Cambodia.”
Ndiye panya wa kwanza kuwahi kushinda tuzo ya ushujaa na heshima ambayo hapo awali ilikuwa imetengwa kwa ajili ya mbwa pekee.
Ukubwa wa panya wa Kiafrika waliofugwa huwawezesha kutembea katika maeneo ya migodi bila kufyatua vilipuzi na kwa kasi zaidi kuliko binadamu aliye na kigunduzi cha chuma.
Mwaka jana, APOPO ilifanikiwa kuwafunza panya 20 na kuwapeleka Cambodia ili kuendeleza kazi ya kugundua vilipuza katika maeneo yaliyokuwa na migodi.
Kwa mujibu wa Kituo cha Utekelezaji cha Migodi ya Cambodia (CMAC), bado kuna mabaki takriban milioni 6 ya vilipuzi ambavyo viko ardhini vinavyotakiwa kuteguliwa.
Panya wa Tanzania wamekuwa maarufu duniani hasa katika shughuli za kugundua na kutegua mabomu ikiwemo nchini Msumbiji.