Mengi awasili Kilimanjaro, Majaliwa kuongoza mazishi yake kesho

Familia ya Mengi wakiwemo watoto wake wakimsindikiza mpendwa wao katika safari yake ya mwisho duniani. Picha|Mtandao
- Tayari mwili wa mfanyabiashara huyo umewasili mkoani Kilimanjaro na kupokelewa na wakazi wa mkoa huo ambapo mazishi yatafanyika kesho kijijini kwake Nkuu, Machame.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa anatarajiwa kuongoza mazishi ya Mwenyekiti Mtendaji wa makampuni ya IPP, Dk Reginald Mengi yatakayofanyika kesho Mei 9, 2019 Machame, wilayani Hai mkoa wa Kilimanjaro.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Majaliwa ataongoza mazishi hayo kwa niaba ya Serikali ambapo ibada ya mazishi itafanyika katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) la Kisereni, Machame na baadaye atazikwa katika makaburi ya familia.
Mwili wa marehemu Mengi tayari umewasili mkoani Kilimanjaro ukitokea jiji la Dar es Salaam ambapo ulipokelewa katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kwa ndege ya shirika la ndege la Precision Air .
Baada ya kuwasili, msafara wa magari yaliyowabeba waombolezaji na mwili wa marehemu umeelekea Machame kwa ajili ya taratibu za mazishi.
Mapokezi ya Mengi katika uwanja wa KIA yaliongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira na viongozi wengine wa Serikali wakiwemo wakuu wa wilaya na viongozi wa kijamii.
Mengi alifariki dunia mjini Dubai, Falme za Kiarabu usiku wa kumkia Mei 2, 2019 na mwili wake uliwasili Mei 6 ambapo jana mfanyabiashara huyo alipewa heshima za mwisho katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam.
Soma zaidi:
- Mengi kuwekeza Sh68 uchimbaji mafuta, gesi Tanzania
- Rais Magufuli, watanzania wamlilia Mengi
- Mengi alivyoacha alama ya uwekezaji katika teknolojia Tanzania
Jana Mei 7, Rais John Magufuli aliwaongoza wakazi wa jiji hilo kumuaga Mengi huku watu waliokuwepo katika eneo hilo wakimuelezea kwa namna tofauti hasa mchango wake aliouacha katika ujenzi wa uchumi wa nchi kwa kutoa nafasi za ajira kwa watu mbalimbali.
Mamia ya wakazi wa Machame wamejitokeza kumpokea mpendwa wao, kuonyesha jinsi alivyoacha alama katika mioyo yao.
Karibu tena Machame Baba,lakini safari hii unarudi ukiwa umelala, #Ican, #Imust, #Iwill itaendelea kuwa ni kauli mbiu inayoishi ndani ya mioyo ya watoto hawa.
Nenda Baba nenda#RIPDrMengi
pic.twitter.com/cK4Y7m1UKV— ITV (@ITVTANZANIA) May 8, 2019
Latest