Mapato mauzo nje ya nchi yapaa, dhahabu ikiongezeka kwa asilimia 42
- Mapato ya jumla ya mauzo ya nje ya nchi yameongezeka kwa takriban asilimia 12.
- Mapato ya dhahabu yapaa kwa takriban asilimia 42 hadi Sh4.92 trilioni.
- Mapato ya mauzo yatokanayo na korosho yaporomoka yakichochewa na kuporomoka kwa bei soko la dunia.
Dar es Salaam. Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imesema mapato yatokanayo na mauzo ya dhahabu nje ya nchi yamengezeka kwa asilimia 42 ndani ya mwaka moja katika mwaka unaoishia Novemba 2019 ikichagizwa zaidi na kupaa kwa bei ya bidhaa hiyo katika soko la dunia na kuongezeka kwa kiwango kilichouzwa nje.
Ripoti ya tathmini ya uchumi ya mwezi Desemba 2019 iliyotolewa hivi karibuni na benki hiyo inabainisha kuwa mauzo ya dhahabu nje ya nchi yalifikia Dola za Marekani 2.14 bilioni (Sh4.92 trilioni) Novemba mwaka jana kutoka Dola za Marekani 1.51 bilioni (Sh3.47 trilioni) Novemba 2018.
Mauzo ya dhahabu, kwa mujibu wa ripoti hiyo, yalikuwa ni zaidi ya nusu au asilimia 51.4 ya bidhaa zisizo za mazao ama kwa kimombo ‘non-traditional goods.”
“Ongezeko la kiwango cha dhahabu iliyouzwa nje kwa kiasi fulani limechochewa na hatua za Serikali katika kusimamia shughuli za madini nchini,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo.
Dhahabu ni miongoni mwa bidhaa zilizochochea pia ukuaji wa jumla wa mapato yatokanayo na mauzo ya nje ya nchi kwa mwaka ulioshia Novemba 2019.
BoT imesema kwa ujumla mapato yatokanayo na mauzo nje ya nchi yalipaa kwa asilimia takriban 12 hadi Dola za Marekani 9.53 bilioni (Sh21.92 trilioni) kwa kipindi hicho ikilinganishwa na ilivyokuwa Novemba 2018 kutokana na kuongezeka kwa thamani ya bidhaa zisizo za mazao na huduma.
“Thamani ya bidhaa zisizo za mazao iliongezeka kwa asilimia 31 hadi Dola za Marekani 4.16 bilioni (Sh9.57 trilioni) kwa mwaka ulioishia Novemba 2019 ikichochewa zaidi na mauzo yatokanayo na dhahabu na bidhaa za viwandani,” imesema BoT.
Zinazohusiana:
- Benki Kuu yatoa maagizo kwa watoa huduma ndogo za fedha
- Mapato ya madini yazidi kumpa tabasamu Rais Magufuli
- Jiandae kwa Nukta mpya mwaka 2020
BoT imesema kuwa uuzaji wa bidhaa za viwandani nje ya nchi nao umepaa badada ya thamani ya mauzo kuongezeka kwa asilimia 28.4 hadi Dola za Marekani 996 milioni (Sh2.29 trilioni) Novemba 2019 ikilinganishwa na ilivyokuwa kipindi kama hicho mwaka juzi.
Hata wakati mapato ya jumla ya mauzo ya nje ya nchi yakiongezeka, mapato yatokanayo na bidhaa za mazao yameendelea kushuka huku yakisinyaa kwa asilimia 21.4 hadi Dola za Marekani 740.3 (Sh1.7 trilioni) katika mwaka ulioishia Novemba 2019.
“Thamani ya mauzo ya mazao yote nje ya nchi ilishuka ukiachana na kahawa, pamba na katani. Kuongezeka kwa mapato yatokanayo na mauzo nje ya nchi ya kahawa, pamba na katani kulichangiwa zaidi na kupaa kwa kiwango kilichouzwa kutokana na hali ya hewa nzuri wakati wa msimu wa mazao hayo,” inasomeka sehemu ya ripoti hiyo.
“Hata hivyo, thamani ya mauzo ya korosho nje ya nchi ilishuka kutokana na kuporomoka kwa bei ya zao hilo katika soko la dunia.”
Latest