Majaliwa awapa Watanzania somo la hisa
Waziri Mkuu Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi nahodha wa timu ya soka ya benki ya CRDB ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo, Abdulmajid Nsekela, kikombe cha ushindi wa mechi ya soka ya kirafiki kati ya timu hiyo na timu ya Bunge iliyochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, Juni 16, 2019. CRDB ilishinda 3-1. Picha|Ofisi ya Waziri Mkuu.
- Amewashauri kujiwekea akiba kwa kununua hisa katika taasisi za fedha.
- Wametakiwa kukopa katika taasisi hiyo kwa ajili ya maendeleo.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka Watanzania kujenga utamaduni wa kujiwekea akiba kwa kununua hisa kupitia taasisi za kifedha kwa ajili ya kuendeleza shughuli za kiuchumi.
Majaliwa aliyekuwa akizungumza jana (Juni 16, 2019) wakati wa bonanza kati ya Wabunge na watumishi wa benki ya CRDB lililofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, amesema suala la wananchi kujiwekea akiba ni muhimu kwa ajili ya maendeleo yao.
“Nashauri wananchi tutumie taasisi za fedha kujiwekea akiba pamoja na kukopa mikopo kwa ajili ya maendeleo yetu,” anasema Majaliwa.
Zinazohusiana:
- M-pesa, intaneti vyachangia Vodacom Tanzania kupata faida ya Sh90 bilioni
- Wawekzaji wa Acacia soko la hisa Dar tabasamu tupu
Akizungumzia kuhusu bonanza hilo lililoandaliwa na benki ya CRDB, Waziri Mkuu amesema michezo ni sehemu nzuri kujenga afya, furaha na kujenga mshikamano wa karibu baina ya benki hiyo na wananchi ambao ni wateja.
Michezo iliyochezwa katika bonanza hilo ni mpira wa miguu ambapo timu ya CRDB ilishinda baada ya kuifunga timu ya Bunge penati tatu kwa moja (3-1).
Kwa upande wa mchezo wa mpira wa pete timu ya Bunge iliibuka na ushindi baada ya kuibugiza CRDB magoli 35 kwa mawili.
Katika mchezo wa kuvuta kamba timu ya Wabunge Wanawake na Wanaume waliibuka na ushindi baada ya kuzishinda timu za CRDB.
Latest