Maandalizi ujenzi mradi wa Stiegler’s Gorge yavuka asilimia 40
Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani akisikiliza maelezo kutoka kwa mkandarasi anayesimamia ujenzi wa mradi wa umeme wa mto Rufiji mkoani Pwani. Picha|Wizara ya NIshati.
- Mradi huo utazalisha megawati 2,115 katika maporomoko ya mto Rufiji na kuondoa tatizo la umeme nchini.
- Mkandarasi anaendelea na ujenzi wa kambi ya muda ya wafanyakazi, usafirishaji wa vifaa na mitambo itakayotumika wakati wa ujenzi pamoja na kazi za kuchukua sampuli za udongo na maji kwa ajili ya utafiti.
Dar es Salaam. Waziri wa Nishati, Dk Medard Kalemani amesema kazi mbalimbali za maandalizi ya ujenzi wa mradi wa umeme wa Stiegler’s Gorge utakaozalisha megawati 2,115 katika maporomoko ya mto Rufiji zimefikia zaidi ya asilimia 40.
Mradi huo unasimamiwa na mkandarasi wa kampuni ya ubia ya Arab Contractors na Elsewedy Electric za nchini Misri ambapo kukamilika kwake kutasaidia kupunguza tatizo la umeme nchini.
Dkt Kalemani aliyekuwa akitoa taarifa ya mradi huo kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ambao walitembelea eneo la mradi lililopo wilayani Rufiji, Mkoa wa Pwani jana, amesema mkandarasi huyo ameanza kazi za maandalizi mara baada ya kukabidhiwa eneo hilo mwezi wa Pili mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa ya Wizara ya Nishati, miongoni mwa kazi ambazo mkandarasi anaendelea kutekeleza kwa sasa ni ujenzi wa kambi ya muda ya wafanyakazi, usafirishaji wa vifaa na mitambo itakayotumika wakati wa ujenzi pamoja na kazi za kuchukua sampuli za udongo na maji kwa ajili ya utafiti.
Mara baada ya kukamilisha kazi hizo za maandalizi mkandarasi huyo anatakiwa kumaliza kazi ya ujenzi ndani ya miezi 36.
Dk Kalemani amesema pamoja na kuridhishwa na hatua hiyo ya maandalizi, bado Serikali itaendelea kumsimamia mkandarasi ili amalize kazi ndani ya muda uliopangwa na wananchi wapate huduma ya umeme kwa wakati.
Soma zaidi:
- Megawati 300 za umeme wa upepo kuchagiza ukuaji wa viwanda Tanzania.
- Rais Magufuli akosoa ripoti ya mazingira Stiegler’s Gorge
Wajumbe wa kamati hiyo ya Bunge pia wamekagua miundombinu wezeshi iliyotekelezwa na Serikali ikiwemo barabara, umeme, nyumba za wafanyakazi na sehemu maalum ya kushushia mizigo katika Stesheni ya Tazara katika Kituo cha Fuga.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati na Madini, Dunstan Kitandula mara baada ya kukagua kazi za maandalizi zinazofanywa na mkandarasi amesema kamati hiyo pia inafuatilia kwa karibu utekelezaji wa mradi huo ili uweze kukamilika kwa wakati kutokana na umuhimu wake nchini.
Amewataka wafanyabiashara hapa nchini kuchangamkia fursa zinazopatikana katika mradi kwa sababu Serikali itatumia takribani Sh6.5 trilioni kutekeleza mradi huo hivyo ni muhimu watanzania wafaidike na fedha hizo.