Kiongozi mbio za mwenge agoma kuzindua mizani ya malori Mwanza

July 5, 2021 10:36 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Hiyo ni baada ya kunusa harufu ya “ufisadi”.
  • Inadaiwa mzabuni wa mradi huo anadai Sh70 milioni na siyo Sh82 milioni.
  • Fedha haziendani na mradi wenyewe wa kujenga mizani ya malori.

Mwanza. Kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa kwa mwaka 2021, Luteni Josephine Mwambashi amegoma kuzindua mradi wa mizani ya malori katika soko la Kirumba Wilayani Ilemela, Mkoa wa Mwanza kutokana na kunusa harufu ya “ufisadi”.

 Ameiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kufanya uchunguzi wa zaidi ya Sh373 milioni  zilizowekezwa katika mradi huo ambapo amebaini kuwepo kwa fedha ambazo hazikutumika vizuri.

Mwambashi amesema kuwa mradi huo una mapungufu ambayo yanahitaji kufanyiwa uchunguzi ikiwemo madai ya zaidi ya Sh82 milioni zinazodaiwa na mzabuni hesabu ambayo inatofautiana na taarifa ya mhasibu wa halmashauri inayoonyesha mzabuni huyo anadai Sh70 milioni.

Madai mengine ni kutoonekana kwa nyaraka muhimu ikiwemo barua ya mzabuni aliyeshinda tenda ya kutekeleza mradi huo pamoja na kutoandaliwa kwa ripoti maalum ya kuanza na kukamilika kwa mradi huo.

“Kutokana na kasoro hizo tulizozipata ninamuomba mhusika wa Takukuru  achukue taarifa hizo kwa ajili ya kuanza uchunguzi wa matumizi ya fedha kwenye mradi huo mara moja,”amesema Mwambashi.

Ameitaka Takukuru kufanya uchunguzi wa kina na kuchukua hatua stahiki kwa mtu yeyote aliyebainika katika ubadhirifu huo.

Amesema kwa muda mfupi waliotumia kwenye mradi huo hesabu ambazo zimeainishwa hapo ni tofauti na zile walizozipata wao ambapo kati ya Sh373 za ujenzi wa mradi huo gharama zilizobainika kutumika ni Sh261.1 milioni.

“Ukitoa na gharama zingine za orientation ambazo ni Sh16 milioni kuna Sh95.17 milioni zinabaki hewani,” amesema mwambashi alipotembelea mradi huo uliokamilika mwaka 2019.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW