Kinachofuata baada ya kina Mbowe kukutwa na kesi ya kujibu
- Wataanza kujitetea Machi 4, 2022.
- Wanausidia kuwa na mashahidi 22.
- Washtakiwa hao wanakabiliwa kesi ya ugaidi.
Dar es Salaam. Baada ya Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi kuwakuta na kesi ya kujibu Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na wenzake watatu, wataanza kujitetea Machi 4, 2022 katika kesi ya ugaidi inayowakabili.
Washtakiwa wengine katika kesi hiyo yenye mashtaka sita ni Halfan Bwire Hassan, Adamu Hassan Kasekwa maarufu kama Adamoo na Mohamed Ling’wenya.
Leo Ijumaa Februari 18, 2022 Jaji Joachim Tiganga anayesikiliza kesi hiyo namba 217 ya mwaka 202o, amesema baada ya kupitia ushahidi wa mashahidi 13 wa Jamhuri na vielelezo, mahakama imeona washtakiwa wote wanne wana kesi ya kujibu.
Akitoa uamuzi huo mdogo, Jaji Tiganga amesema baada ya mahakama kupitia vielelezo hivyo na mashahidi vilivyotolewa kuthibitisha makosa yanayowakabili na baada ya kujiridhisha imeona washitakiwa wote wana kesi ya kujibu katika shtaka la kwanza hadi la tano.
Katika shtaka la sita, mahakama imesema hawana kesi ya kujibu kwa sababu hakukuwa na vielelezo vya kutosha kuthibitisha tuhuma hizo.
Soma zaidi:
-
Jaji Siyani ajitoa kesi ya Mbowe na wenzake, atoa maelekezo
-
Polisi wasema Mbowe anahojiwa Dar es Salaam kwa makosa ya jinai
-
Mbowe na wenzake watatu wakutwa na kesi ya kujibu
Uamuzi uliofanywa leo na Jaji Tiganga umekuja baada ya upande wa Jamhuri kukamilisha kuwasilisha ushahidi wake wiki hii kupitia mashahidi wake 13 kati ya 24 waliotarajiwa kutoa ushahidi mahakamani.
Bada ya uamuzi huo, Wakili anayeongoza jopo la upande wa utetezi, Peter Kibatala akaiomba mahakama kuwa washtakiwa hao waanze kujitetea Machi 4, 2022.
Pande zozote mbili zimeridhia tarehe hiyo ya washtakiwa waanze kujitetea na Jaji Tiganga ameahirisha kesi hiyo hadi Machi 4.