Kesi za kodi: Mpina awagonganisha vichwa mawaziri bungeni
- Ahoji kwa nini mashauri 1,097 ya kodi hajaamuliwa mpaka.
- Mawaziri wapata kigugumizi watoa majibu tofauti na swali.
- Spika aagiza wajipange na kuleta majibu sahihi.
Dar es salaam. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba na Naibu wake Hamad Hassan Chande wamejikuta katika wakati mgumu leo bungeni baada ya kutokuwa na majibu ya uhakika kuhusu kesi zilizopo mahakamani zinazohusu madai ya kodi.
Utata huo umejitokeza leo Bungeni katika kipindi cha maswali na majibu Septemba 22, 2022 baada ya Mbunge wa Kisesa Luhaga Mpina kutaka kujua kwa nini kesi 1,097 za kodi zenye thamani ya Sh360 trilioni na Dola za Marekani milioni 181.4 hazijaamuriwa hadi sasa.
Hata hivyo, Naibu Waziri Hamad katika majibu amesema hadi Agosti 2022 kulikuwa na mashauri 854 yenye thamani ya Sh4.21 trilioni na Dola za Marekani milioni 3.48.
“Mashauri hayo pamoja na mapya yanayosajiliwa yanaendelea kusikilizwa katika taasisi za rufani za kodi ambazo ni Trat na Trab. Aidha kwa nyakati tofauti mashauri ya kodi hupungua au kuongezeka kulingana na kasi ya usikilizaji na usajili,” amesema Hamad wakati akimjibu Mpina.
Moto ukawaka
Baada ya majibu hayo Mpina alipopewa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza, alimuambia Spika Dk Tulia Ackson hajajibiwa kile alichouliza katika swali la kwanza.
“Nasikitika kwamba swali limeuliza trilioni 360 lakini nimejibiwa trilioni 4.21,” amesema Mpina.
Hali hiyo ikamuinua Spika Ackson na kuwataka mawaziri kufafanua uhalali wa swali la Mpina kwani majibu yaliyotolewa hayaendani na swali lililoulizwa.
“Nataka kuelewa kwanza hapa haya mashauri haya ndiyo mashauri yaliyopo ambayo Serikali inayajua tofauti na ya mbunge au mmechagua kati ya yaliyopo na mmeamua kutolea majibu,” amehoji Spika Tulia na kumtaka Waziri Nchemba kutolea ufanunuzi kabla hajampa fursa naibu wake kutoa maelezo.
Soma zaidi:
Dk Nchemba amewaambia wabunge kuwa Sh360 trilioni si za madai ya kikodi yanayoendelea katika taasisi za rufani za kikodi bali ni madai ya makinikia.
Hata hivyo, Spika wa Bunge amesema kutokana na kutofautiana kwa majibu ya Serikali na swali la msingi lililoulizwa na Mpina, mawaziri hao waandae majibu kadri ya swali lilivyoulizwa.
“Natoa fursa hili swali likajibiwe yeye Mpina anavyotaka majibu, kama yeye hayuko sahihi ndio swali langu lilikuwa hapo, haya majibu siyo ya swali lake,” ameagiza Spika.