Hapa ndipo waombaji wa kazi hukwama wakiitwa kwenye “interview”

January 30, 2020 12:29 pm · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Baadhi yao hukosa mvuto, utashi wa vitu walivyoviandika kwenye wasifu (CV).
  • Uwezo wa kujieleza na kujiamini bado ni changamoto kwa waombaji wengi wa kazi.
  • Vijana wengi wanashindwa kujifunza maarifa mapya yanayohitajika wakati wa mahojiano.

Dar es Salaam. Huwa ni furaha kwa mwombaji wa kazi, pindi anapopokea  ujumbe mfupi kwenye simu au barua pepe yake kuwa, “Hongera! Maombi yako ya kazi yamepokelewa na umechaguliwa kuingia katika awamu ya pili ya mahojiano (interview) ambayo itafanyika siku ya…”

Kwa wengi ambao wameomba kazi kwa muda mrefu bila mafanikio, ujumbe huo huamsha furaha na matumaini makubwa ya kupata kazi. 

Lakini hali hubadilika baada ya kufanya mahojiano na kuambiwa kuwa utaitwa mchakato wa kuchambua wasifu wako utakapokamilika. Wengi husubiri kwa muda mrefu bila kupata majibu. Kwa tafsiri nyingine unakuwa umekosa vigezo vya kuajiriwa. 

Yapo mambo mengi yanayosababisha ushindwe kuvuka katika hatua hii muhimu ya mahojiano ikiwemo kukosa kujiamini na mawasiliano yaliyodhorota wakati wa mahojiano (interview). 

Nukta (www.nukta.co.tz) inakuletea mambo ambayo waajiri wanatumia kama vigezo vya msingi wakati wa mahojiano ili mtu apate fursa ya kuajiriwa ambayo mtu anapaswa kuzingatia ili atoboe: 

Uwiano baina ya mwombaji na wasifu wake

Wakati baadhi ya vijana wakifikiri kujaza wasifu wao (CV) kwa kurasa kede kede ni ujanja kiasi cha kudanganya ili waonekane kuwa wana uzoefu kwenye nyanja nyingi, waajiri wamesema hilo ni jambo linalofanya watu wengi kushindwa kupata kazi. 

Meneja wa kiwanda cha kusaga unga na bidhaa lishe za mifugo cha Lina Mills, Christian Kulwa amesema mbali na mfululizo wa vijana wengi kuomba kazi ambazo hazipo kwenye fani zao, wengi hata wakifikia kwenye hatua ya mahojiano hawajua chochote kuhusu kazi waliyoomba.

“Unakuta mtu CV imeshiba, amefanya kila aina ya kazi anayoitafuta kwenye kampuni yako. Unajisemea, “Multi task” si ndiyo huyu lakini lo! Mpe kompyuta hata kutafuta programu ya “Microsoft Exel” hajui,” amesema Kulwa.

Waombaji wa kazi wanashauriwa kuandika kwenye CV zao kile walichonacho na wanachokijua vizuri na hata wakipewa kazi wanaweza kufanya bila ubabaishaji. Epuka ujanja ujanja wa kutaka mambo makubwa usiyoyaweza. 

Hakikisha kile ulichokiandika kwenye wasifu wako kinaendana na ujuzi na uwezo ulionao kutekeleza kazi unayoomba ili kuepuka usumbufu wakati wa mahojiano. Picha| Christina @ wocintechchat.com|Unsplash.

Kushindwa kujieleza

Mkufunzi wa waajiriwa na waajiri,  Moses Samora amesema moja kati ya swali ambalo vijana wengi hushindwa kulielezea vizuri ni swali la “jieleze wewe ni nani?”. 

Wakati waajiri wakitegemea mtu atoe maelezo ya jinsi elimu yake ilivyomsaidia na itakavyomsaidia katika kazi anayoomba, watu wengi huwashangaza watu wanaowahoji kwa kujielezea walikotokea, hali yao ya uchumi na zaidi maisha yao binafsi.

“Unanielezea umezaliwa Longido ukachunga ng’ombe mimi inanihusu nini? Ninategemea uniambie umesoma chuo fulani ukajitolea sehemu fulani ambapo umejifunza moja, mbili tatu. Mengine hayanihusu,” amesema Samora.

Kama hujui jinsi ya kujieleza wewe ni nani, soma mtandaoni vitu vya msingi unavyotakiwa kuvitaja wakati ukijieleza mbele ya wanaokuhoji. 

Matumizi ya lugha isiyofaa

Vijana wengi wamezoea kutumia lugha ya mtaani na maneno yasiyo rasmi kiasi cha kujikuta wakiyatumia hata kwenye kipindi cha mahojiano ya kazi. Hiyo ni moja kati ya vitu vinavyowaondolea sifa ya kupata kazi.

Mbali na kushindwa kutumia lugha moja wakati wa mahojiano, mara kadhaa waombaji wengine hujikuta wakikosea matamshi ya maneno ya Kiingereza ambacho wanachanganya na Kiswahili.

“Uliza mtu ulikuwa unafanya nini kabla ya kuomba kazi hii. Utasikia mtu anasema alikua “Intaprinyua” badala ya kusema “enterpreneur” kwa maana ya mjasiriamali.

“Mtu kama huyu unakuta ameomba kazi ya kuwa meneja ambayo ni kazi inayohusisha kukutana na watu wengi wenye heshima zao na hata wageni, hatuwezi kuajiri mtu atakayetuaibisha,” amesema Kulwa.

Kabla hujaingia katika chumba cha mahojiano ni vema kufahamu lugha ambayo utahojiwa nayo na ujiweke sawa na kuhakikisha unaongea kwa ufasaha bila ubabaishaji ili uaminiwe katika kile unachoongea. 


Zinazohusiana:


Jiongeze kwa maarifa na ujuzi

Hata baada ya sayansi na teknolojia kutafuna kazi nyingi, baadhi ya vijana wameshindwa kukubaliana na hali hiyo kwa kushupaa katika kujiongezea maarifa ya kujua vitu vingi zaidi ya vile walivyosomea. 

Mkurugenzi wa Nkamba General Supplies, Mathias Kitulla amesema kwenye kutafuta waajiriwa katika hoteli yake alipata changamoto ya watu wengi kukosa ujuzi na uwezo wa kufanya kazi ya moja (multi task).

“Hivi kweli mtu unashindwa kujiongezea maarifa unabaki na kitu kimoja tu ulichosomea unategemea nini? Kwenye karne hii, tumia fursa yoyote ya kujifunza inayokuja mbele yako,” amesema Kitulla.

Hivyo ni kusema, ni muhimu kujiendeleza katika kila unachokifanya ili kuwa na uwezo wa ziada au kama kile alichokisema Kitulla, “Outshining others.”

Muonekano wako (First impression)

Hakikisha kabla hujaenda katika mahojiano ya kazi, vaa nguo zenye muonekano mzuri kwako na kwa wale wanaokuhoji. Muonekano wako wa kwanza wakati wa mahojiano ni muhimu sana kukuelezea wewe ni nani.

Afisa Utawala wa kampuni ya uendelezaji wa ujasiriamali wa teknolojia ya  Seedspace Dar es Salaam, Lilian Mgeni amesema muonekano wa kwanza ni moja kati ya vitu ambavyo waajiri wengi huangalia kwa mtu ambaye anatarajiwa kujitambulisha kama mmoja wa waajiriwa wa kampuni.

“Mara nyingi tunaangalia jinsi mtu anaweza kujieleza kwa watu, namna ya uvaaji wake na hata aina ya lugha anayotumia,” amesema Mgeni.

Baadhi yao hukosa mvuto, utashi wa vitu walivyoviandika kwenye wasifu (CV), jambo linalowakwamisha kupata kazi za ndoto zao. Picha| LinkedIn Sales Navigator/Unsplash.

Kukosa uelewa wa majukumu ya kazi anayoiomba

LIilian amesema, wakati tangazo linatolewa kutafuta mtu maalumu kwa kazi fulani, matangazo mengi huandika majukumu yanayotarajiwa kufanywa na mtu huyo.

Licha ya vijana “kutafuniwa” bado wanashindwa kujielezea majukumu watakayoyafanya pale swali hilo likiulizwa. Nadharia hiyo inaacha maswali kwa waajiri juu ya umakini wa mtu atakayeshindwa kujibu swali hilo.

“Wengi wanatumia muda mwingi kutaka kujielezea hata wasiyoulizwa, mtu hata huna uelewa wa kazi uliyoomba wala majukumu yake sasa unatarajiaje kupigiwa simu?,” amehoji Mgeni.

Naye Samora amesema, vijana wengi huenda kutafuta ajira wakiwa hawajui hata masomo waliyosomea yanaweza kutumika katika kazi zingine. Wengi kama wamesomea sheria basi wanataka kufanya sheria pekee.

“Wengi wanashindwa kufanya udadisi na kupanga mpango mkakati kufahamu kuwa kazi hii naifanya, kazi hii nafanya na hii kwa kweli ipo nje ya kisomo changu,” ameelezea Samora.

Ninatumaini hautofanya makosa haya pale unapoenda kwenye mahojiano ya kazi na utakua umejibiwa maswali ya kwanini ulikuwa unafanya mahojiano lakini baada ya kumaliza hupati kazi licha ya kuamini kuwa ulijieleza vizuri. 

Usikae mbali na ukurasa huu kujua ni kwanini waajiri hawatoi majibu baada ya kupokea maelfu ya bahasha za watu wanapoomba kazi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW