Filamu ya Fatal Affair: Kiboko kwa wachepukaji

July 19, 2020 5:31 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link

David na Ellie wanaonjeshana penzi walilopeana miaka 20 iliyopita lakini linaingia doa hata kabla halijanoga. Picha|Mtandao.


  • Inamuhusu mwanadada Ellie ambaye alichepuka mara moja tu na kujikuta akiwindwa na mchepuko wake.
  • Hofu inatanda pale mume wake anapoanza kupata mashaka kama Ellie yupo sawa.
  • Visa vitimbi na sintofahamu za hapa na pale, ni sehemu tu ya filamu hii ya saa moja na nusu.

Dar es Salaam. Hapa ndipo chozi linapoanza kudondoka. Pale unapochepuka na mchepuko ukakolea na mahaba yako!

Mke na mama wa mtoto mmoja, Ellie (Nia Long) anajikuta kwenye njiapanda baada ya kuchepuka kwa usiku mmoja tu na kujikuta akicheza mchezo wa kifaranga na kicheche.

Licha ya kuwa safari ya ukumbusho na mchepuko huyo haikufika “Galilaya”, haha! Wakubwa wameelewa, bado haikuwa rahisi kwa David (Omar Epps) kusahau mahaba mazito aliyopata kwa mwanamama Ellie.

Safari ilianza hivi…

“Ellie,”aliita David baada ya kumuona mrembo ambaye alioneka kuwa na historia naye ya muda mrefu ndani ya gauni ambalo linaweza kukufanya ukatike shingo kwa kugeuka kumtazama.

“David! Habari yako,” alisema Ellie huku akielekea alipo David ambaye suti imemkaa kana kwamba amechongwa nayo.

“Umekuwa ni muda mrefu huh!”, Ellie alisema “Miaka 20. Inabidi tuonane” David alikazia.


Zinazohusiana:


Usiku wa kuonana uliwadia wawili hao waliuanza kwa kunywa mvinyo. 

“Unaonekana unaishi ndoto yako, labda kama kuna shida peponi,” David alimchokoza Ellie.

Naye bila kuujua mtego huo alijikuta akimfungukia rafiki huyo wa muda mrefu siri za ndoa yake na jinsi mume wake anashindwa kumkamilisha.

“Siku moja unaamka na mtu aliyelala pembeni yako anakuwa kama mtu usiyemfahamu,” Elle anayasema hayo kwa David ambaye anaiona hiyo kama fursa.

Usiku unavyoenda, wawili hao wanabadili kiwanja na kwenda sehemu watakapokumbushia miaka 20 iliyopita.

Lo! David hawezi kuvumilia kulikosa penzi la binti ambaye alimpenda miaka 20 iliyopita lakini akashindwa kumuambia. 

Glasi ya kwanza inazaa nyingine na nyingine na nyingine tena. Lakini ebo, hata wakati wakianza kujikumbushia safari yao kama wapenzi wakumbukavyo, yaani kuelekea kule kusikopaswa, Ellie anakumbuka kuwa ni mama na ni mke kwa Michael (Stephen Bishop) na hivyo kuikatiza safari hiyo.

Hakuna siri inayoweza kufichika na hakuna uongo unaoweza kukaa gizani hapo ndipo “Fatal Affair” inapozaliwa.

David ambaye hataki kuacha penzi hilo liende bila kukamilika, anajikuta akimuwinda Ellie na familia yake. Hapo ndipo watu wanapopigana chupa na kusababisha vifo ili tu David apate penzi lisilo lake.

Maisha ya nani yatapotea, je, Michael atajua? Fuatilia mkasa huu kupitia mtandao wa Netflix kama tu kifurushi chako kimelipiwa. 

Wikiendi ndiyo hiyo, inaanza.

Enable Notifications OK No thanks