Elimu, afya bora ndiyo msingi wa maendeleo endelevu Tanzania-Benki ya Dunia
Mkurugenzi Mkaazi wa benki hiyo nchini Tanzania, Bella Bird aliyekuwa akizungumza leo (Julai 18, 2019) jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa taarifa ya uchumi wa Tanzania (Tanzania Economic Updates). Picha|Kwanza TV.
- Benki hiyo imeitaka Tanzania kuongeza uwekezaji ili kujenga mtaji wa watu wenye afya na ujuzi wa kuifikisha katika uchumi wa kati ifikapo 2025.
- Serikali yasema itaendelea kuboresha miundombinu ya elimu na afya.
Dar es Salaam. Benki ya Dunia imeitaka Tanzania kuongeza juhudi za kuwekeza katika elimu na afya za wananchi wake ili kujenga mtaji wa watu wenye afya na ujuzi wa kuifikisha katika uchumi wa kati ifikapo 2025.
Mkurugenzi Mkaazi wa benki hiyo nchini Tanzania, Bella Bird aliyekuwa akizungumza leo (Julai 18, 2019) jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa taarifa ya uchumi wa Tanzania (Tanzania Economic Updates), amesema uwekezaji huo unapaswa kuelekezwa zaidi kwa watoto na vijana ambao wanahitajika katika shughuli za maendeleo endelevu.
“Kwa nchi kufikia ukuaji na umoja endelevu, inahitaji kufanya uwekezaji kwa watu wake, kwa sababu mtaji wa binadamu ni mali muhimu zaidi ya nchi yoyote,” amesema Bird.
Amesema uwekezaji huo ni kuendeleza juhudi kubwa zilizofanyika katika uboreshaji wa afya na elimu ili kuhakikisha unachangia katika kuifikisha nchi katika uchumi wa katika Ifikapo 2025.
Aidha, amebainisha kuwa uboreshaji wa miundombinu ya elimu na afya nayo ni muhimu ili kuwapatia fursa watoto na vijana kuwa na elimu na afya njema itakayowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo.
Lakini imetakiwa kuboresha mazingira mazuri ya biashara kwa ajili ya sekta binafsi hasa wawekezaji wanaowekeza katika sekta mbalimbali zinazogusa maisha ya wananchi ambao ndiyo msingi mkuu wa maendeleo wa nchi yoyote.
Taarifa hiyo ni sehemu ya ripoti ya mradi wa Benki ya Dunia wa rasilimali watu (HCI) unaolenga kuzihimiza nchi mbalimbali duniani kuwekeza zaidi kwa wananchi wake ambapo unajikita zaidi katika kuangalia afya za watoto chini ya miaka mitano, ubora wa elimu inayotolewa shuleni; uendelezaji wa uchuzi kwa vijana na kuzuia udumavu kwa watoto.
Soma zaidi:
- CHATI YA SIKU: Kinachofahamika kuhusu utekelezaji wa bajeti ya Serikali mwaka 2017-2018
- Sababu zilizofanya Tanzania iporomoke viwango vya ufanyaji biashara duniani
- Benki ya Dunia yaridhia kutoa mkopo wa zaidi ya Sh600 bilioni: Ikulu
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Faustine Ndungulile amesema taarifa hiyo iliyozinduliwa leo itawasaidia kufanya tathmini ya maeneo muhimu ya kuboresha ili kuhakikisha afya za Watanzania zinakuwa sehemu ya maendeleo ya Taifa.
“Tunakubali tuna changamoto lakini tumejipanga kuhakikisha tunatengeneza mifumo itakayosaidia kuendeleza rasilimali watu,” amesema Dk Ndungulile.
Ripoti hiyo ya HCI inaeleza kuwa kukosekana kwa usawa wa kijinsia bado ni kikwazo kwa Tanzania kuendeleza kipato na rasilimali watu hasa katika maeneo ya kazi na elimu.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, William Ole Nasha amesema Serikali itaendelea kuboresha ubora wa elimu ikiwemo kuongeza uwekezaji katika miundombinu ya kufundishia na walimu kwa kuongeza bajeti inayopangwa kila mwaka.
Amesema kwa mwaka wa fedha wa 2019/2020, asilimia 20 ya bajeti yote imeelekezwa katika sekta ya elimu ili kuongeza ujuzi na nguvukazi ya Taifa kwa kuwapatia wanafunzi na vijana maarifa na ujuzi unatakiwa katika soko la ajira.