DSE yaongeza ukomo mabadiliko ya bei hisa za CRDB hadi 10%
- Uongozi wa DSE umeongeza mara mbili wigo wa ukomo wa mabadiliko ya bei kwa hisa kwa siku kutoka asilimia 5 hadi 10 ndani ya siku tano za kazi.
Dar es Salaam. Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) limeongeza kwa muda ukomo wa mabadiliko ya bei ya hisa za benki ya biashara ya CRDB kutoka asilimia tano hadi asilimia 10 kwa siku baada ya benki hiyo kutangaza gawio kwa wawekezaji wake.
CRDB (CRDB Bank PLC) imetangaza leo gawio la Sh90 kwa hisa kwa mwaka wa fedha 2025 baada ya kuripoti faida baada ya kodi ya Sh724.6 bilioni, ikiwa ni kiwango cha juu kurekodiwa tangu kuanzishwa kwa benki hiyo miaka 30 iliyopita.
Gawio hilo, lililopendekezwa na Bodi ya Wakurugenzi ya CRDB, ni ongezeko la asilimia 38 ndani ya mwaka mmoja kutoka gawio la Sh65 kwa hisa lilitolewa mwaka 2024, jambo litakalowaacha wawekezaji hao na tabasamu.
Katika taarifa yake kwa umma iliyotolewa leo Aprili 15, 2026, uongozi wa DSE umesema kuwa ongezeko hilo la ukomo wa mabadiliko ya bei ya hisa litakuwa kwa siku tano za kazi kuanzia leo Aprili 15 hadi 21, 2026.
Kwa mujibu wa kanuni za DSE, bei ya hisa kwenye soko hilo hairuhusiwi kupanda au kushuka kwa zaidi ya asilimia tano kwa siku moja ya biashara.
“Soko linahifadhi haki kuchukua hatua nyingine zozote zitakazoonekana zinafaa kuhakikisha kuwa soko linaendeshwa kwa utulivu na utaratibu mzuri unadumishwa,” imesema taarifa ya DSE.
Mara nyingi kampuni iliyoorodheshwa kwenye soko la hisa ikitangaza gawio huwa kuna presha baina ya wawekezaji ya kutaka kununua na kuuza hisa kutokana na kiwango cha gawio husika.
Katibu wa kampuni wa CRDB Pascal Mihayo amewataka wawekezaji kuwasilisha na kusasisha taarifa zao za malipo katika matawi yaliyo karibu, tovuti ya Benki, App ya CRDB Investor na makao makuu ya CRDB Bank.
Latest