Darasa la saba kikaangoni kesho, Necta ikionya udanganyifu wa mitihani

October 6, 2020 11:41 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Mtihani huo utafanyika kwa siku mbili kuanzia kesho Oktoba 7 hadi 8, 2020 katika shule 17,335 za Tanzania Bara. 
  • Jumla ya wanafunzi milioni 1.02 watafanya mtihani huo ambapo kati yao, 530,718 ni wasichana sawa na asilimia 51.83.
  • Necta yasema itachukua hatua za kisheria kwa watakaohusika na wizi na udanganyifu wa mitihani.  

Dar es Salaam. Wakati watahiniwa wa darasa la saba wakitarajia kuanza mitihani ya kumaliza elimu ya msingi kesho, Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta) limewaonya wanafunzi, walimu na wasimamizi kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu na wizi wa mitihani. 

Mitihani hiyo itafanyika kwa siku mbili kuanzia kesho Oktoba 7 hadi 8, 2020 katika shule 17,335 za Tanzania Bara.

Watahiniwa hao watafanya mitihani hiyo katika masomo matano ya Kiswahili, Hisabati, Kiingereza, Sayansi na Maarifa ya Jamii.

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde aliyekuwa akizungumza jijini Dar es Salaam leo (Oktoba 6, 2020) amesema jumla ya wanafunzi milioni 1.02 watafanya mtihani huo ambapo kati yao, 530,718 ni wasichana sawa na asilimia 51.83 ya watahiniwa wote.

Dk Msonde amesema kati ya watahiniwa hao, 2,943 ni wenye mahitaji maalum wakiwemo wenye ulemavu wa kuona 86 na wasiosikia 739. 


Zinazohusiana:


Aidha, Necta imeonya kuhusu vitendo vyovyote vya udanganyifu na wizi wa mitihani na kuwa yeyote atakayegundulika kushiriki vitendo hivyo atachukuliwa hatua kali za kisheria.

Dk Msonde amewataka wasimamizi, watahiniwa, walimu, wamiliki wa shule na wananchi wote kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu na kwamba watahiniwa watakaobainika watafutiwa matokeo yao.

“Kamati zote za mitihani za mikoa, halmashauri na manispaa nchini zinatakiwa kuhakikisha kwamba taratibu zote zinazohusika na uendeshaji wa mitihani ya Taifa zinazingatiwa ipasavyo. 

“Kamati zote zinaagizwa kuhakikisha mazingira yote ya vituo vya mitihani yako salama, tulivu kuwawezesha watoto wetu kufanya mitihani kwa amani kabisa,” amesema Katibu Mtendaji huyo.

Pia Necta haitasita kukifuta kituo chochote cha mtihani endapo itajiridhisha kuwa kuwapo kwake kunahatarisha usalama wa mitihani ya Taifa.

Dk Msonde amesema tahadhari hiyo inatoa matarajio kuwa wanaohusika, wakiwamo wanafunzi, walimu, wasimamizi na vituo, watazingatia misingi iliyowekwa na Necta, hivyo kamati zihakikishe mazingira ya mitihani hayaruhusu udangajifu wowote kutokea.

Maandalizi yote ikiwemo usambazaji wa mitihani katika maeneo husika umekamilika. 

Mwaka jana, Necta ilifuta matokeo ya watahiniwa 909 waliofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2019 kwa sababu mbalimbali ikiwemo  udanganyifu.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW