CCM yaahidi kuendelea kufungua fursa za kiuchumi Morogoro
- Yaahidi Sh bilioni 2.6 kama mikopo kwa wanawake, vijana na wenye ulemavu.
Dar es Salaam. Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeahidi kuendelea kufungua fursa za kiuchumi katika mkoa Morogoro ikiwa kitapata ridhaa ya kuongoza tena nchi kwa kipindi cha miaka mitano ijayo.
CCM iliyozindua kampeni zake kitaifa jana jijini Dar es Salam imetoa ahadi hizo kupitia mgombea wake wa nafasi ya urais, Samia Suluhu hassan aliyekuwa akinadi sera za chama hicho leo Agosti 29, 2025 Ngerengere, mkoani Morogoro.
Miiongoni mwa ahadi za mgombea huyo ikiwa atapata ridhaa ya kuongoza kwa miaka mitano ijayo ni kutoa mikopo kwa ajili ya kundi la wanawake , vijana na wenye ulemavu.
“Tutahakikisha kila kijana, kila mwanamke na kila mtu mwenye ulemavu anapata nafasi ya kuinua kipato chake. Tutatoa Sh bilioni 2.6 kama mikopo kwa wanawake, vijana na wenye ulemavu wapatao 8,320 ili kuwaongezea mitaji kwa ajili ya kujinyanyua kiuchumi.” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amewaahifi wakazi wa Ngerengere kuwa Serikali yake itakamilisha ujenzi wa barabara ya Bigwa–Mvuha–Kisaki ndani ya miaka mitano ijayo ili kufungua fursa za kilimo na biashara ikiwa watapata ridhaa ya kurudi tena madarakani.
Mbali na shughuli za kiuchumi cahama hicho kimeahidi kukamilika kwa miradi ya maji ili kuondoa kabisa kero ya ukosefu wa huduma hiyo, ujenzi wa vituo vipya viwili vya afya, zahanati saba na kukamilisha ujenzi wa zahanati nyingine nne zinazoendelea kujengwa sambamba na kuhamasisha wananchi kujiunga na bima ya afya ya Taifa.
Ziara ya Rais Samia Ngerengere ni muendelezo wa kampeni za kitaifa ambazo zimeanza rasmi jana, Agosti 28, baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kumthibitisha kuwania urais.