Bunge lampitisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais kwa asilimia100
- Ndejembi amepata kura 324 kati ya ya kura 324 za wabunge zilizopigwa, sawa na asilimia 100 ya kura zote ambazo kati yake hakukuwa na kura zilizoharibika wala kura za hapana.
Dar es Salaam. Bunge la Tanzania limemthibitisha Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania ikiwa ni siku mbili tu tangu Rais Samia kupendekeza jina lake kufuatia kujiuzulu kwa Dk Emmanuel Nchimbi kwenye nafasi hiyo.
Hatua hiyo imefikiwa leo Agosti 28, 2026 mara baada ya kukamilika kwa mchakato wa kikatiba uliowataka wabunge wa Bunge la Tanzania kupiga kura kupitisha mteule huyo wa Rais ndani ya siku 14 baada ya nafasi ya Makamu wa Rais kuwa wazi.
Kwa mujibu wa Spika wa Bunge Mussa Azzan Zungu, Ndejembi amepata kura 324 kati ya kura 324 za wabunge zilizopigwa, sawa na asilimia 100 ya kura zote ambazo kati yake hakukuwa na kura zilizoharibika wala kura za hapana.
Makamu wa tatu kwa Rais Samia
Kwa sasa, Ndejembi anasubiri kuapishwa rasmi hapo kesho Agosti 29, 2029 ili aanze kutekeleza majukumu yake katika nafasi hiyo.
Iwapo ataapishwa, atakuwa Makamu wa Rais wa tatu kuhudumu chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, hatua itakayomfanya Rais Samia kuwa rais aliyewahi kuwa na Makamu wa Rais wengi zaidi katika historia ya Tanzania.
Akizungumza baada ya kuthibitishwa, Ndejembi amesema yuko tayari kutumikia dhamana aliyopewa kwa Watanzania akieleza kuwa utendaji wake hautopimwa kwa umri mdogo alionao bali uadilifu wake na utekelezaji wa kazi atakazotumwa.
“Dhamana hii haitapimwa kwa udogo wangu pekee, wala haitopimwa kwa udogo wangu kabisa, dhamana hii itapimwa kwa uadilifu kwa Watanzania, dhamana hii itapimwa kwa kazi yoyote nitakayotumwa kuitekeleza,” amesema Ndejembi anayekwenda kuwa Makamu wa Rais mwenye umri mdogo zaidi katika historia ya Tanzania.
Katiba imevunjwa?
Hata hivyo, uteuzi na kuthibitishwa kwa Ndejembi siku saba kabla ya Septemba 4, 2026, tarehe ambayo Dk Nchimbi alisema ataachia rasmi madaraka, kumeibua mjadala wa kikatiba kuhusu iwapo hatua hiyo inamaanisha moja kwa moja kwamba Dk Nchimbi amepoteza nafasi ya kuendelea kuwa Makamu wa Rais, au ataendelea kushikilia wadhifa huo hadi Septemba 4, 2026, siku aliyotangaza kuwa ataachia madaraka rasmi.
Kabla ya Agosti 26, 2026, Chama cha Mapinduzi kutangaza kumfukuza uanachama kwa madai ya kukiuka Katiba, kanuni na taratibu za chama, Wakili Peter Majanjara kutoka Chika Attorneys aliiambia Nukta Habari kuwa siku 14 za kikatiba zinazotoa nafasi ya kufanyika kwa mchakato wa kumpata Makamu wa Rais Mpya zingeanza kuhesabiwa kuanzia Septemba 4.
Hata hivyo, leo bungeni Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Hamza Johari amesema kufuatia kufukuzwa uanachama Dk Nchimbi amepoteza sifa za kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania.
Johari anasema kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania, Ibara ya 47(4) inayoeleza sifa za mtu anayetakiwa kuwa Makamu wa Rais, mtu hawezi kuwa kiongozi wa kisiasa kama hatoki kwenye chama chochote cha siasa.
Hivyo tangu Dk Nchimbi kutangazwa kufukuzwa uanachama kiti kiko wazi, na Ndejembi kupendekezwa kushika nafasi hiyo, Tanzania iko katika siku 14 za kikatiba za kumpata Makamu wa Rais mpya.
“Taarifa imekuja kwamba aliyekuwa Makamu wa Rais amevuliwa uanachama, kwa hiyo akivuliwa uanachama hiyo sifa mojawapo hapo imeondolewa,” amesema Johari akitoa ufafanuzi.